
Chuo cha Muziki wa nchi za Jahazi (DCMA) ni shirika linalotoa elimu ya muziki lililoanzishwa mnamo mwaka 2001.
DCMA ilianzisha shule ya muziki katika Mji Mkongwe mnamo mwaka 2002 na kutoa mafunzo ya muziki pamoja na mafunzo ya ala mbalimbali za muziki kwa bei nafuu kwa mtu yeyote yule ambaye anapenda kujifunza muziki ama kuwa mahiri katika ala mbalimbali za muziki.
DCMA hasa imeweka msisitizo katika kufundisha aina mbalimbali za muziki wa asili ya Zanzibar kama vile Taarab, Beni na Kidumbaki na walimu walio wengi ni kutoka hapa Zanzibar. Aidha, chuo cha muziki kinaendesha warsha, mafunzo na semina maalum za muziki kwa kushirikiana na walimu mbalimbali kutoka nje ya nchi ili kuongeza umahiri na ujuzi kwa wanamuziki wanao shiriki mafunzo kutoka katika chuo hiki.
Chuo kina sehemu kubwa sita ambazo ni:
* Mafunzo ya muziki kama: Violin, Oud, Qanun, Cello na Gita
* Mpango wa ufadhili kwa wanafunzi
* Librari ya muziki (inatoa vyombo vya muziki kwa matumizi ya hapa chuoni pamoja na noten za muziki, mashairi pamoja na kurekodi)
* Mafunzo kwa vikundi vya muziki (Muziki kutoka Zanzibar na nchi za majahazi, Muziki wa Kimagharibi, pamoja na ngoma za asili)
* Kutafuta nafasi kwa wanamuziki kwa ajili ya kuwatangaza na kutafuta kazi ndani na nje ya nchi
* Warsha na semina
Chuo cha Muziki kinatoa nafasi ya kutunza na kuendeleza azina kubwa ya utamaduni na muziki wa asili ya Zanzibar na kutoa elimu ya nadharia na elimu ya ufundi.
Chuo cha Muziki cha Zanzibar, DCMA, kinapenda kutoa taarifa inayohusu maonyesho ya muziki katika maeneo ya wazi katika manispaa ya Zanzibar na onyesho moja kubwa la kufunga muhula (URITHI 2010) yatakayofanyika siku ya tarehe 26 Julai 2010 pale Lebanoni Mtaa wa Baghani, tarehe 27 Julai 2010 pale Michenzani mbele ya Jumba namba 2 na tarehe 30 Julai katika chuo cha muziki “DCMA” katika barabara ya Mizingani mkabala na Makumbusho ya Kasri.
Maonyesho hayo ni sehemu ya mkakati wa chuo katika kupeleka mafanikio yaliyopatikana kwa jamii pamoja na wageni wakaazi na wageni wote waishio hapa Visiwani Zanzibar. Maonyesho hayo yatafanyika katika mpangilio ufuatao:
Julai 26, 2010- saa 10:30 alaasiri mpaka 11:30 alaasiri Lebanon Square-Mji Mkongwe
Onyesho la Muziki wa Taaarab asilia litafanyika Lebanon Square likishirikisha walimu na wanafunzi wa muziki kutoka DCMA. Onyesho hilo lina lengo la kupeleka ladha halisi ya Taarab asilia kwa wakaazi wa maeneo ya Lebanoni pamoja na wageni na watu wote kwa ujumla.
Julai 27, 2010- saa 10:30 alaasiri mpaka 11:30 alaasiri Michenzani mbele ya Jumba namba 2
Onyesho la Muziki mchanganyiko kutoka katika bendi ya wanafunzi “Swahili Vibe” kutoka DCMA. Bendi ya Swahili Vibe inajulikana kwa kupiga muziki mchanganyiko na wenye ladha tofauti, kuanzia Muziki wenye asili ya mwambao wa Pwani ya Bahari ya Hindi na muziki kutoka pande mbalimbali za Tanzania na Afrika kwa ujumla.
Onyesho hilo litakuwa limesheheni vibaji kutoka “DCMA” Aidha, onyesho hilo litakuwa na lengo kubwa la kupeleka muziki kwa jamii ili kushajiisha wakaazi wa Visiwa vya Zanzibar wenye vipaji na nia ya kujifunza muziki kuweza kuitumia nafasi hiyo kupata taarifa mbalimbali kuhusu chuo na shughuli zake katika kuendeleza muziki unaojali tamaduni na asili ya Zanzibar.
Mbali na kufanya maonyesho hayo, “DCMA” itafanya onyesho kubwa la kumaliza muhula Julai 30, 2010 kuanzia saa 2 usiku hapa chuoni DCMA. Onyesho la URITHI 2010 ni mfululizo wa maonyesho ya muziki kutoka hapa chuoni yanayofanyika kila mwaka.
Onyesho hilo ni la mwisho wa muhula na litafanyika katika sehemu zote za jengo la chuo. Watazamaji watapata nafasi ya kipekee ya kuona aina mbalimbali za muziki wenye vionjo vya sauti mbalimbali vyenye ladha halisi kuanzia ghorofa ya tatu ya jengo mpaka sehemu ya chini ya jengo ambapo onyesho la mwisho litafanyika.
Ungana nasi katika safari hii ya kipekee ili kuona vipaji vya muziki vya hali ya juu kutoka katika Chuo cha muziki wa nchi za Majahazi “DCMA”
Maonyesho hayo yamedhaminiwa na Vodacom Tanzania, Pemba Lodge, Mnarani Beach Cottage, Zan Air na Zanzibar Grand Palace.
Tunaambatanisha bango la kutangaza maonyesho hayo sambamba na taarifa hii kwa ajili ya matumizi yako.
Tunaomba hisani ya kuchapishwa taarifa hii. Kwa maelezo zaidi tafadhali wasiliana nasi kupitia anwani ifuatayo: -
Dismas Leonard Sekibaha
Development, Marketing & PR Manager
Dhow Countries Music Academy, Zanzibar
press@zanzibarmusic.org