Wakati huo huo, Rais
Jakaya Mrisho Kikwete Jumatatu, Novemba 29, 2010, amemtembelea hospitali na kumjulia hali mwanamuziki mkongwe wa Tanzania, Bwana Muhidin Gurumo, ambaye amelazwa kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Bw. Gurumo ambaye amelazwa Wodi Mosi, Mwaisela, amekuwa hospitalini hapo tokea Alhamisi iliyopita, Novemba 25, 2010, akisumbuliwa na ugonjwa wa shinikizo la damu.
Rais Kikwete amekaa na mwanamuziki huyo kwa kiasi cha dakika 15 na baadaye madaktari bingwa wa moyo wa MNH wamethibitisha kuwa hali ya Bw. Gurumo imetulia na kuwa akiendelea na hali ya sasa anaweza kutolewa hospitali wiki ijayo.
Rais Kikwete ambaye baada ya kumjulia hali Bw. Gurumo alitaka kumtembelea na kumjulia hali mwanamuziki mwingine, Bw. Remmy Ongala, ambaye naye amelazwa kwenye hospitali hiyo kwa matatizo ya figo.
Hata hivyo, Rais Kikwete amejulishwa kuwa Bw. Ongala wakati huo alikuwa nje ya wodi yake kwa ajili ya kufanyiwa vipimo katika sehemu nyingine ya hospitali hiyo. Bw. Ongala naye amelazwa Wodi ya Sita, Mwaisela hiyo hiyo.
Kwa miaka mingi, wanamuziki hao wawili wenye vipaji vikubwa vya muziki wametamba katika muziki wa Tanzania. Bw. Gurumo amekuwa nyota wa muziki katika Tanzania tokea miaka ya 1960 na amepigia ama kuongoza baadhi ya bendi maarufu za muziki katika Tanzania zikiwamo za NUTA (baadaye JUWATA na OTTU) ambayo sasa inaitwa Msondo Ngoma Music Band, Orchestra Safari Sound (OSS) na DDC Mlimani Park (Sikinde).
Naye Ongala kwa miaka mingi aliongoza bendi ya Super Matimila, kabla ya kuingia katika muziki wa Gospel.