Na Frank Geofray, Jeshi la Polisi
 Maofisa na askari Polisi kote nchini  wametakiwa kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi kwa kuwa suala hilo siyo la hiari bali ni la lazima kulingana na kanuni pamoja na taratibu za ufanyaji wa kazi za Polisi.
 
 Hayo yalisemwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Said Mwema, wakati wa kikao cha kikazi kilicho wakutanisha maofisa wa Polisi Makao makuu, Kanda maalumu ya Dar es Salaam na Vikosi vya Jeshi hilo chenye lengo la kuwajengea uwezo na kupeana mafunzo yatakayosaidia kufanya kazi kwa weledi zaidi ili kuweza kukabiliana na vitendo vya uhalifu wa aina mpya unaojitokeza hapa nchini katika sura mbalimbali.
 
Aidha, IGP Mwema alisema, kila ofisa na askari polisi anapaswa kutekeleza kwa vitendo utoaji wa huduma bora ndani na nje, ikiwa na maana kwa askari wenyewe na kwa wananchi, ili kuendana na maboresho yanayoendelea ndani ya Jeshi hilo na kuweza kukabiliana na vitendo vya vurugu na matishio mengine ya kihalifu na wahalifu yanayojitokeza hapa nchini.
 
Aliwatataka Makamanda na maofisa wa polisi wote kuendelea kuwa karibu na wananchi ili kujua kero za kiusalama zinazowakabili na kwa pamoja kuweza kuzitafutia ufumbuzi ili kuondoa hofu ya uhalifu kuanzia ngazi ya familia hadi Taifa jambo ambalo litaendelea kuimarisha hali ya usalama hapa nchini.
 
Aidha Mwema, amesema Jeshi la Polisi halitasita kuwachukulia hatua kali baadhi ya watu wanaotumia mwamvuli wa siasa au dini kama kisingizio cha  kufanya ama kuchochea vurugu hapa nchini kwa kuwa vurugu hizo ni kosa la jinai kama yalivyo makosa mengine ya jinai.
 
“Hakikisheni mnawakamata wale wote wanaofanya vitendo vya vurugu kwa visingizio vya siasa kwa kuwa siasa zao zinaishia pale tu wanapokuwa wamefanya vitendo vya vurugu ambavyo ni kosa la jinai na sisi hatuwezi kuwafumbia macho” Alisema Mwema.
 
IGP Mwema alisema Jeshi la Polisi litaendelea kufanya kazi zake kwa kufuata kanuni, maadili na taratibu zinazoliongoza katika kuhakikisha amani na usalama vinadumu hapa nchini na kusisitiza kuwa askari wa Jeshi la polisi si wanachama wa chama chochote cha siasa japokuwa wanaruhusiwa kupiga kura.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. AnonymousMay 22, 2013

    I like this guy (IGP) he is very humble just like Kamanda Mpinga, God bless you two. Laiti kama polisi wote wangeiga mfano wa hawa tungekuwa mbali.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...