Makundi mawili maarufu ya muziki wa kizazi kipya nchini TMK family na Tip Top Connections wanatarajiwa kupamba mechi za ligi kuu Vodacom ya Simba na Yanga na ile ya Azam FC dhidi ya JKT Ruvu inayochezwa kesho Jumamosi jijini dar es salaam.

Uwepo wa burudani hizo ni sehemu ya mkakati wa mdhamini mkuu wa ligi hiyo kampuni ya huduma za mawasiliano ya simu za mkononi ya Vodacom ya kuhitimisha msimu wa ligi wa 2013/2014 kwa kishindo na burudani ya aina yake.

Meneja Uhusiano wa Nje wa Vodacom Salum Mwalim amesema kundi la Tip Top Connections likinogeshwa na msanii mahiri Ma D litaipamba mechi ya watani wa jadi ya Simba na Yanga kwenye uwanja wa taifa huku TMK wanaume family wakiwasindikiza washabiki wa mabingwa Azam FC kwenye uwanja wa Azam Complex

 "Tumeamua kuifunga ligi yetu kwa mtindo wa aina yake kwa kutoa burudani kwa mabingwa wapya Azam FC pamoja na kuipamba mechi ya Yanga ambao walikuwa mabingwa watetezi na washindi wa pili wa msimu huu tunaoumalizia"Alisema Mwalima katika taarifa yake kwa vyombo vya habari

 Mwalim amesema mechi zote mbili zinatarajiwa kuvutia hisia za maelfu ya wapenda soka nchini kutokana na kila mechi kuwa na umuhimu wake katika historia na rekodi za soka nchini na hivyo ni wazi maelfu ya washabiki watafurika kwenye uwanja wa Taifa na Azam Complex huku wengine wakifuatilai mechi hizo kupitia matangazo ya moja kwa moja ya redio na Luninga

 "Mechi zote mbili ni muhimu sana huku Azam akitaka kuweka rekodi ya kumaliza msimu bila ya kupoteza mchezo huku timu zenye utani wa jadi za Simba na Yanga zikishuka dimbani huku kila mmoja akitaka kulinda heshima mbele ya mwezake"Aliongeza Mwalim.

 Mwalim amesema maandalizi yote kwa upande wao wameyakamilisha na kwamba kilichobakia sasa ni kwa washabiki kufika uwanjani ili kuona ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara inavyohitimishwa kwa mbwembwe za aina yake.

Amesema katika mechi hizo, Vodacom itakabidhi kombe kwa mabingwa wapya Azam FC pamoja na medali kwa timu ya Yanga na Mbeya City zinazomaliza nafasi ya pili na ya tatu katika msimamo wa mwisho wa ligi hiyo.

 "Wakati wote tunaangalia ni vipi tunaweza kufanya mambo yatakayoinogesha ligi hii kuu ya Vodacom, na hivyo ni imani yetu kwamba makundi haya mawili ya burudani ni sahihi na yanahadhi inyoendana na ligi na michezo husika,"Aliongeza Mwalim

 Burudani katika viwanja vyote viwili inatarajiwa kuanza mapema majira ya saa saba ili kutoa nafasi nzuri kwa washabiki kupata burudani yakutosha kabla ya kuanza kwa mechi majira ya saa kumi alasiri

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...