Katibu wa CCM Mkoa Mjini
Mohammed Omar Nyawenga akitoa taarifa ya Chama hicho kwa Waandishi wa Habari
kuhusu kujitoa ndani ya Chama Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa katika
mkutano uliofanyika Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui.
Baadhi ya wanachama wa Chama
cha Mapinduzi wakifuatilia mkutano huo uliofanyika Afisi Kuu ya CCM aKisiwandui
Mjini Zanzibar.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa Mjini
Borafia Silima akitoa ufafanuzi katika mkutano uliohudhuriwa na wajumbe wa
ngazi mbali mbali za Chama na waandishi wa Habari Afisi kuu ya CCM Kisiwandui
Mjini Zanzibar.
Na Mwashungi Tahir/Maryam
Kidiko -Maelezo Zanzibar
Chama cha Mapinduzi (CCM)
kimesema ni Chama kikubwa chenye wafuasi na wanachama wengi pamoja na
Viongozi wenye hekima, busara, mapenzi na uadilifu mkubwa.
Hayo yameelezwa na
Katibu wa CCM Mkoa Mjini Mohammed Omar Nyawenga wakati alipokuwa
akitoa taarifa kwa Waandishi wa Habari kuhusu kujitoa Chama cha
Mapinduzi Waziri Mkuu
wa zamani Edward Ngoyai Lowassa na kujiunga na Chama cha upinzani huko
Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui
Amesema CCM ni Chama kinacho aminiwa na kukubalika na Wananchi
wengi wa Tanzania hivyo kujitoa kwa mwanachama mmoja ama kikundi cha
wanachama haiwezi kukiathiri chama
hicho.
Nyawenga ameongeza kuwa wingi
wa wanachama wa chama hicho haujaletwa
na utajiri wa vingozi wake bali umetokana na uimara wa Siasa, Sera na itikadi
yake.
Alisema CCM haina hasara
kumpoteza mwanacham mmoja anaetaka kubadili sera na itikadi ya Chama kwa maslahi yake binafsi na marafiki zake hata
kama utajiri wake ni mkubwa wa kupindukia.
Ameongeza kuwa uwamuzi wa
Lowassa kujiondowa ndani ya Chama hicho sijambo la kukishituwa chama, viongozi,
pamoja na wanachama wake na hakiwezi kudhoofika wala kutetereka.
Alisema hii sio mara ya
kwanzi kwa Chama cha Mapinduzi kuondokewa na kiongozi mwandamizi na kujiunga na
vyama vya upinzani na bado kinaendelea kuimarika.
“Mwaka 1989, CCM iliwafukuza
uanachama viongozi waandamizi 11 akiwemo Waziri Kiongozi mstaafu wa Zanzibar
Seif Sharif Hamad, akafuatia Agostino Lyatonga Mrema na mwaka jana CCM ilimfukuza uanachama
aliyekua Mwakilishi wa Kiembesamaki Mansour Yussf,” alikumbusha Katibu wa Chama
Mkoa.
Nyawenga aliweka wazi
kuwa umaarufu alionao Lowassa inawezekana umejengwa kutokana na CCM
lakini haiwezekani umaarufu wa Chama hicho umejengwa kutokana na yeye.
Alisema wanachama wa Zanzibar
waliokuwa wakimuunga mkono Lowassa katika
azma ya kuomba kuteuliwa na CCM kuwa
mgombea wa kiti cha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania walifanya hivyo kwa
sababu ya siasa, sera na ilani ya Chama na sasa baada ya kuhama wameamua kujitenga na hawako pamoja naye.
Mwenyekiti wa Mkoa wa Mjini Magharib
Borafia Silima amesema kwamba Tanzania inaheshimika kuwa ni nchi
yeye amani, na mshikamano na Chama cha Mapinduzi kinafuata utaratibu wa katiba iliyowekwa.
Amesema kila Mwanachama anayo
haki na uhuru wa kuchaguwa kiongozi
anayemtaka na yeye kuchaguliwa na mtu
yeyote ikiwa ni Demokrasia iliyotandikwa na Chama hicho.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...