Kiongozi wa shirikisho la soka barani Afrika Issa Hayatou (pichani) kutoka Cameroon amepewa jukumu la kuongoza shirikisho la soka duniani Fifa kwa muda.
Hayatou atachukua usukani kufuatia kusimamishwa kazi kwa Rais wa Fifa Sepp Blatter kwa muda wa siku 90 na Kamati ya Maadili ya shirikisho hilo,
Shirikisho hilo linalosimamia soka duniani limesema kupitia taarifa.
Hayatou, aliyeongoza CAF tangu 1988, atachukua usukani kwa mujibu wa sheria za Fifa, akiwa ndiye makamu wa rais katika kamati tendaji ya Fifa aliyehudumu muda mrefu zaidi.
Baadaye, Hayatou ametoa taarifa na kusema amepokea majukumu hayo mapya lakini ataongoza tu kwa muda.
“Rais mpya atachaguliwa kwenye Mkutano Mkuu Februari 26, 2016. Na mimi mwenyewe sitawania,” amesema kupitia taarifa.
“Hadi mkutano huo ufanyike, naahidi kwamba nitajitolea kwa nguvu zangu zote kutumikia shirikisho hili, mashirikisho wanachama, waajiri wetu, washirika na mashabiki wa soka popote walipo.”
Aidha, ameahidi kuendelea kushirikiana na watawala na kuendeleza uchunguzi kwenye shirikisho hilo lililoyumbishwa na madai ya ulaji rushwa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...