Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman amemshukuru Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli kwa kutimiza ahadi
yake ya kuipatia Mahakama kiasi cha shilingi Bilioni 12.3 alizoahidi wakati wa
maadhimisho ya Siku ya Sheria Februari 4, 2016 jijini Dar es salaam.
Amesema Fedha hizo zitatumika katika utekelezaji wa miradi
mbalimbali ya maendeleo ikiwemo uboreshaji wa miundombinu ya Mahakama na ujenzi
wa Mahakama mpya katika maeneo mbalimbali nchini.
Akitoa shukrani hizo leo jijini Dar es salaam Mhe.Othman amesema
kuwa kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2012 Mahakama imepata asilimia 100 ya fedha
zote za Maendeleo zilizokasimiwa na Bunge kwenye Bajeti yake ya mwaka
2015/2016.
Amesema kupatikana kwa fedha hizo ambazo ni za Maendeleo
kutasaidia kufufua miradi ya ujenzi iliyosimama, kufufua Mahakama ambazo
zilikua hazifanyi kazi kwa sababu ya uchakavu na kuipatia Mahakama fursa zaidi
ya kutoa huduma bora kwa wananchi kwa kuwasogezea huduma za Haki karibu katika
maeneo wanayoishi.
Mhe.Othman ameeleza kuwa kwa kipindi cha bajeti za miaka 3
mfululizo kuanzia mwaka 2012 /2013 hadi 2014/2015 Mahakama ilikua
ikipokea fedha pungufu ya kiasi kilichopangwa katika Bajeti hali iliyochangia
kuzorota kwa shughuli za Mahakama.
” Kwa mara ya kwanza Mahakama tumepata asilimia 100 ya Bajeti yetu
ya mwaka 2015/2016 kutoaka Serikalini, mwaka 2012/2013 tulipata shilingi
bilioni 26.9 ikiwa ni pungufu ya bajeti yetu kwa asilimia 78, mwaka 2013/2014
tukapata Bilioni 42.7 pungufu kwa asilimia 82 na mwaka 2014/2015 tulipewa
shilingi bilioni 41.5 ambayo ni pungufu kwa asilimia 92 “
Akizungumzia miradi ya ujenzi wa majengo mapya ya Mahakama amesema
kuwa tayari Mahakama ina michoro ya ramani za majengo yatakayojengwa katika
maeneo mbalimbali ambayo hayakuwa na huduma hiyo ikiwemo mikoa 12 kati ya 25
ambayo haina Mahakama Kuu, wilaya 22 kati ya 133 ambazo hazina Mahakama za
Wilaya pamoja na kuongeza Mahakama za Mwanzo ambazo ziko 976 kufikia kata zote
3,957.
Kuhusu Mradi wa ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya
Mahakama utakaofanyika katika uwanja wa Chimala jijini Dar es salaam
amesema utahusisha maeneo mbalimbali ya utoaji huduma za Kimahakama
na kuongeza kuwa Mahakama itajenga jengo lenye viwango kwa
kuwatumia Wakandarasi na wataalam wa kitanzania watakaojenga
Mahakama nzuri na yenye viwango kwa gharama nafuu.
“Mahakama tutatoa kipaumbele kwa wataalam wetu wa ndani ili waweze
kutujengea Mahakama zetu, tunalenga kuwafikishia huduma zetu katika maeneo
wanayoishi tunao mfano mzuri wa Mahakama ya mwanzo ya Dumila iliyoko
Morogoro, Mahakama hii imejengwa kijijini ni ya kisasa” Amesisitiza
Mhe.Othman.
Kwa upande wake Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Harrison Mwakyembe
amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na Mahakama ya Tanzania ili
kuwezesha ufanisi wa shughuli zake kwa kuhakikisha kuwa kiwango cha fedha za
Bajeti kinachopitishwa kwa ajili ya kuhudumia shughuli za Mahakama
kinafika kwa wakati.
Akizungumzia kuhusu uanzishwaji wa Mahakama ya Mafisadi, amesema
uanzishwaji wake uko katika hatua nzuri na wakati ukifika wananchi
watataarifiwa kama ilivyoahidiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
kuungwa mkono na Mahakama ya Tanzania.
Naye Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango,
akizungumzia fedha za Maendeleo zilizotolewa na Mhe.Rais amesema kuwa
lengo la ahadi ya Rais kwa Mahakama ilikua ni kuhakikisha Haki inapatikana kwa
wananchi kwa Wakati na kwamba miongoni mwa vitu vilivyokua vikichelewesha haki
kwa watanzania walio na mashauri Mahakamani ni ukosefu wa fedha na uchakavu wa
miundombinu.
Amesema Serikali inaendelea kujenga uwezo wa kifedha ili
kuimarisha huduma katika mihimili yote ikiwemo Bunge na Mahakama huku msisitizo
ukiwekwa katika kukusanya mapato ya ndani.
“Kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) tuna dhamira
ya dhati ya kukusanya mapato ya ndani ili kujenga uwezo wa Serikali tutawabana
wote waliokuwa wanakwepa kulipa kodi na hili tutalisimamia kikamilifu”
Amesema utoaji wa Haki ni moja ya ukuzaji wa maendeleo ya nchi na
kuongeza kuwa Mahakama ya Tanzania inafanya kazi nzuri pamoja na ufinyu wa
bajeti yake.
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman akimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli kwa kutimiza ahadi yake ya kuipatia Mahakama kiasi cha shilingi Bilioni 12.3. zitakazotumika katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo uboreshaji wa miundombinu ya Mahakama na ujenzi wa Mahakama mpya katika maeneo mbalimbali nchini. Kulia ni Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Harrison Mwakyembe na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango (kushoto).
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman akimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli kwa kutimiza ahadi yake ya kuipatia Mahakama kiasi cha shilingi Bilioni 12.3. zitakazotumika katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo uboreshaji wa miundombinu ya Mahakama na ujenzi wa Mahakama mpya katika maeneo mbalimbali nchini. Kulia ni Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Harrison Mwakyembe na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango (kushoto).
Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Harrison Mwakyembe (wa pili kutoka kushoto) akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa Habari kuhusu Serikali kuendelea kushirikiana na Mahakama ya Tanzania ili kuwezesha ufanisi wa shughuli zake.
Shukran za dhati na pongezi za pekee kwa Mh. Rais wetu J.P. MAGUFULI kwa kuitimiza ahadi yake kwa vitendo kama alivyoahidi. Nanyi wahusika tunaamini mtayatekeleza yale yote mliyoorodheshana kuweza kupatiwa kiasi hicho cha fedha ili kuyatimiza. Kumbukeni, Mh. Rais kama alivyosema katika ile hotuba yake, ifikapo siku kama ile, atakuja kuwauliza ili apate 'feedback' kuweza kujuwa ni nini kimefanyika na kinachoendelea.
ReplyDeleteBLA BLA NYINGI SASA WAFUNGENI HAO MAFISADI, MARA TU MWEZI MMOJA ATI PESA IMEKWISHA, TUNAWAJUENI VIZURI KUSANYENI HIZO TRILLION MNAZODAIWA NA SEREKALI KAMA MTAFANYA KAZI
ReplyDelete