Na Teresia Mhagama, Mtera
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo ameeleza kuwa Mameneja wa Shirika la umeme nchini (TANESCO) wanaosimamia Kanda mbalimbali nchini wataondolewa katika vyeo hivyo iwapo hawatatimiza maagizo mbalimbali waliyopangiwa na Wizara ya Nishati na Madini ifikapo Machi 1 mwaka huu.
 Waziri wa Nishati na Madini alisema hayo wakati wa kikao chake na watendaji wa Shirika la Umeme nchini (TANESCO) na Taasisi nyingine zilizo chini ya Wizara ya Nishati na Madini kilichofanyika katika Kituo cha kuzalishia umeme cha Mtera.
Profesa Muhongo alitaja maagizo hayo kuwa ni kuunganisha umeme kwa wateja wengi, kuwa na makusanyo makubwa ya bili za umeme, kupunguza manung’uniko ya wananchi katika huduma za umeme na uboreshaji wa mawasiliano kati ya Shirika hilo na wananchi.
“Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, ifikapo Machi Moja mwaka huu atatuthibitishia kama Mameneja hawa wataendelea na majukumu haya wanayoyasimamia ama la na hii itatokana na ufanisi  wa utendaji katika majukumu tuliyowapangia,” alisema Profesa Muhongo.
Aidha,  Waziri wa Nishati na Madini alisema kuwa Kitengo cha Uwekezaji cha Tanesco kama hakitakuwa na miradi mipya ya umeme ifikapo tarehe 2 Aprili mwaka huu, watendaji katika  Ofisi hiyo wataondolewa katika nafasi hiyo kwa kushindwa kutimiza majukumu yake ipasavyo.
“Hapa hatuna mzaha kwani mahitaji ya umeme ni makubwa na tuna miradi mingi ya usambazaji umeme kwa wanannchi ikiwemo miradi ya REA na wananchi wanahitaji umeme kwa matumizi ya majumbani na kuanzisha viwanda vidogodogo, sasa bila miradi mipya ya umeme tutashindwa kusambaza umeme kwa  wananchi hawa kwa kuwa kiasi cha umeme  tulichokuwa nacho sasa bado hakitoshi,” alisema Profesa Muhongo.
Profesa Muhongo pia aliwaasa Mameneja wa TANESCO wa Kanda kuwakaribisha wawekezaji mbalimbali wa umeme ikiwemo miradi midogo ya uzalishaji umeme wa maji ili nchi iwe na umeme wa kutosha na sio kuwakatisha tamaa wawekezaji hao.
Vilevile Profesa Muhongo alisema  kuwa watumishi watakaoleta urasimu katika kujadili masuala ya uwekezaji wa nishati wataachia ngazi kwani ndio wanaokwamisha juhudi za serikali katika kuongeza kiasi cha umeme nchini.
 “TANESCO na EWURA kwa sasa pale anapojitokeza mwekezaji wa miradi ya umeme lazima mjadiliane naye kwa pamoja badala ya mwekezaji husika kwenda TANESCO baadaye anaenda EWURA au TPDC hivyo mwekezaji anapokuja jadilini naye kwa pamoja ili msitumie muda mrefu  katika utekelezaji wa suala moja na hivyo kuchelewesha utekelezaji wa miradi mbalimbali,” alisema Profesa Muhongo.
Vilevile Profesa Muhongo aliwaagiza watendaji wa  TANESCO katika vitengo vya ukaguzi kufanya kazi hiyo kwa ufanisi mkubwa ikiwemo usimamizi madhubuti wa nguzo za umeme ambazo baadhi huanguka kila inapofika msimu wa mvua na kusema kuwa suala hilo halikubaliki.
 Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (aliyesimama) akizungumza na watendaji mbalimbali wa Wizara ya Nishati na Madini na Taasisi zilizo chini ya Wizara wakati wa kikao chake na Watendaji  hao kilichofanyika katika Kituo cha kuzalishia umeme cha Mtera.Kulia ni Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani na kutoka kushoto (mstari wa mbele)  ni Kaimu Kamishna wa Nishati na Maendeleo ya Petroli, Mhandisi Norbert Kahyoza, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo na Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Profesa Justin Ntalikwa.
 Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (aliyesimama) akizungumza na watendaji mbalimbali wa Taasisi zilizo chini ya Wizara wakati wa kikao chake na Watendaji  hao kilichofanyika katika Kituo cha kuzalishia umeme cha Mtera. Kushoto kwa Waziri ni Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani Kutoka kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika  la  Madini la Taifa (STAMICO), Zena Kongoi, Dkt.Wellington Hudson, Mkurugenzi wa Mkondo wa Chini kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dkt. James Mataragio,  Mkurugenzi  wa Umeme, Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Mhandisi Anastas Mbawala na Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Felix Ngamlagosi.

 Watendaji mbalimbali wa Taasisi zilizo chini ya Wizara wakiwa kwenye kikao na Waziri wa Nishati na Madini  Profesa Sospeter Muhongo (hayupo pichani)  kilichofanyika katika Kituo cha kuzalishia umeme cha Mtera. Kutoka kulia ni Dkt.Wellington Hudson, Mkurugenzi wa Mkondo wa Chini kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dkt. James Mataragio,  Mkurugenzi  wa Umeme, Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Mhandisi Anastas Mbawala na Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Felix Ngamlagosi. 
Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Profesa Justin Ntalikwa (aliyesimama) akizungumza katika kikao cha Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo (hayupo pichani) na Watendaji wa Taasisi zilizo chini ya Wizara  kilichofanyika katika Kituo cha kuzalishia umeme cha Mtera.Wengine kutoka kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Dkt. Lutengano Mwakahesya, Naibu Mkurugenzi Kitengo cha Usambazaji na Huduma kwa Wateja Shirika la Umeme nchini (TANESCO), Sophia Mgonja, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Felchesmi Mramba, na Kaimu Kamishna wa Nishati na Maendeleo ya Petroli, Mhandisi Norbert Kahyoza.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...