Na Veronica Simba
Serikali imetoa ridhaa kwa Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM) kufanya uchimbaji wa madini hayo kwa njia ya chini kwa chini (underground mining), sambamba na njia waliyokuwa wakitumia awali ya uchimbaji wa wazi (Open Pit).
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amesaini Kibali kinachoruhusu Mgodi wa GGM kufanya uchimbaji huo wa chini kwa chini, leo Machi 15 katika Ofisi za Makao Makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na Uongozi wa GGM kabla ya kusaini Kibali husika, Waziri Muhongo alimwambia Mkurugenzi Mtendaji wa Mgodi huo, Terry MulPeter kuhakikisha wanatumia utaratibu wa wazi katika kulipa ushuru wa huduma (service levy).
Alisema, wananchi, hususan wanavijiji wanaoishi jirani na Mgodi huo wanayo haki kujua ni kiasi gani kinalipwa na GGM kama ushuru wa huduma kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika vijiji vyao.
“Mtapaswa kuwasilisha Mfano wa Hundi ya malipo, yenye kiasi cha fedha mlichotoa kwa jamii kila mnapolipa ushuru wa huduma ili wananchi wajue ni kiasi gani mmelipa,” alisisitiza.
Vilevile, Profesa Muhongo aliongeza kuwa, wakati wa kukabidhi Hundi hiyo ya mfano, Naibu Waziri wa Nishati na Madini ni lazima awepo kushuhudia zoezi hilo na kama sio yeye basi atawakilishwa na Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Madini.
Alisema, kiongozi mwingine anayepaswa kushuhudia zoezi hilo la kukabidhi hundi ya mfano ya malipo ya ushuru wa huduma kutoka kwenye Mgodi kwenda kwa jamii ni mmoja wa viongozi waandamizi kutoka Serikali ya Mtaa husika.
Kabla ya kusaini Kibali hicho, Profesa Muhongo aliwauliza Kaimu Kamishna wa Madini, Julius Sarota na Kamishna Msaidizi wa Madini, Kanda ya Ziwa Viktoria Mashariki, David Mulabwa kama Mgodi huo umekamilisha taratibu zote zinazopaswa ikiwa ni pamoja na kulipa kodi na tozo mbalimbali za madini kwa wakati, ambapo viongozi hao waliafiki.
“Taratibu zote za kisheria ikiwa ni pamoja na masuala ya uhifadhi wa mazingira zimefuatwa kikamilifu,” alisema Sarota. Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi Mulabwa alimhakikishia Waziri kuwa amejiridhisha na sababu zilizotolewa na Mgodi huo kuomba kibali cha kuchimba chini kwa chini na hivyo hana pingamizi kuhusu ridhaa hiyo kutolewa kwao.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa GGM, MulPeter, akijibu swali la Waziri kuhusu ulipaji wao wa kodi na tozo mbalimbali kwa Serikali, alisema kuwa Mgodi huo umekuwa ukilipa kodi zote stahiki kwa wakati.
“Kwa mwaka huu wa 2016 kwa mfano, tumelipa Dola za Kimarekani Milioni 21.6 kama mrabaha, tumelipa Dola za Kimarekani Milioni 1.6 kama ushuru wa huduma na makadirio ya malipo ya kodi ya mapato kwa mwaka huu ni Dola za Kimarekani Milioni 37,” alisisitiza.
Aidha, Waziri Muhongo alitumia fursa hiyo kuutaka Uongozi wa Mgodi huo kufanya zoezi la utafiti wa madini (exploration) na kubainisha maeneo ambayo yako ndani ya leseni yao lakini hawatayatumia kwa shughuli za uchimbaji ili wapewe wananchi wenye uhitaji kwa ajili ya kufanyia shughuli mbalimbali za kimaendeleo.
Waziri Muhongo alisaini Kibali kinachotoa ridhaa kwa Mgodi wa GGM kufanya shughuli za uchimbaji wa chini kwa chini kupitia Sheria ya Madini ya Mwaka 2010, kifungu cha 48 (3) kinachompa mamlaka hayo Waziri mwenye dhamana na Wizara husika.
Kibali hicho cha kuchimba chini kwa chini kwa Mgodi wa Geita kitatumika katika Mashimo (Pit) ya Star na Comet.
 Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (Kulia), akisaini Kibali cha kuuruhusu Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mine – GGM) kufanya uchimbaji wa madini wa chini kwa chini (underground mining) badala ya uchimbaji wa wazi (Open pit) uliokuwa ukifanywa awali. Anayeshuhudia ni Mkurugenzi Mtendaji wa GGM, Terry MulPeter. Kwa kibali hicho, sasa GGM watafanya uchimbaji kwa njia zote mbili. Waziri Muhongo amesaini Kibali hicho  Machi 15, 2016 Makao Makuu ya Wizara, jijini Dar es Salaam.
 Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (Kulia) akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mine – GGM) Terry MulPeter, Kibali cha Mgodi huo kufanya uchimbaji wa madini wa chini kwa chini (underground mining). Awali, GGM walikuwa wakifanya uchimbaji wa wazi pekee. Kibali hicho kimetolewa, Machi 15, 2016 Makao Makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Mgodi wa Dhahabu wa GGM, Terry MulPeter (Kulia), akimsikiliza Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (Kushoto) wakati wa kikao baina yake na Uongozi wa GGM, kabla ya kusaini Kibali kinachouruhusu Mgodi huo kufanya uchimbaji wa chini kwa chini (Underground mining). Tukio hilo limefanyika Machi 15, 2016 Makao Makuu ya Wizara, jijini Dar es Salaam. Wengine pichani ni baadhi ya Viongozi na Maofisa Waandamizi wa Wizara.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (katikati), akizungumza na Uongozi wa Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mine – GGM) (Kushoto), kabla ya kusaini Kibali kinachouruhusu Mgodi huo kufanya uchimbaji wa chini kwa chini (Underground mining). Kulia ni baadhi ya Viongozi na Maofisa Waandamizi wa Wizara. Waziri amesaini Kibali hicho  Machi 15, 2016 Makao Makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...