Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amefanya ziara yake ya kwanza nje ya nchi leo
tarehe 06 April, 2016 kwa kutembelea nchi jirani ya Rwanda, ambapo yeye na
Mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mheshimiwa Paul Kagame wamefungua Kituo
cha Pamoja cha Utoaji wa Huduma za Mpakani (One Stop Border Post) na Daraja la
Kimataifa la Mto Rusumo katika Mpaka wa Tanzania na Rwanda.
Rais Magufuli ambaye ameongozana na
Mkewe Mama Janeth Magufuli, ameingia nchini Rwanda kwa usafiri wa magari
akitokea nyumbani kwake Lubambangwe, katika kijiji cha Mlimani, Wilaya ya Chato
Mkoani Geita ambako alikuwa mapumziko tangu tarehe 29 Machi, 2016.
Katika eneo la Rusumo, Rais
Magufuli na Rais Kagame kwanza wamefungua majengo ya Kituo cha Pamoja cha
Utoaji wa Huduma za Mpakani kilichopo upande wa Tanzania ,
kisha wakafungua daraja la mto Rusumo, na baadaye wakafungua Majengo ya Kituo
cha Pamoja cha Utoaji wa Huduma za Mpakani kilichopo upande wa Rwanda .
Mradi huu wa ujenzi wa Kituo cha
Pamoja cha utoaji wa Huduma za Mpakani cha Rusumo, umehusisha ujenzi wa majengo
ya mamlaka ya Mapato katika pande zote mbili na daraja lenye urefu wa mita 80
na upana wa mita 9.5, na umegharimu shilingi Bilioni 61.4 zilizotolewa kwa
ufadhili wa serikali ya Japan kupitia shirika lake la JICA.
Akizungumza katika sherehe ya
ufunguzi wa mradi huo Rais Magufuli ameishukuru Japan
kwa kutoa fedha za kuwezesha utekelezaji wa mradi huo na ametoa wito kwa
wafanyabiashara wa Rwanda
kupitisha mizigo yao Tanzania kupitia mpaka huo, pamoja na
kuitumia bandari ya Dar es salaam.
Dkt. Magufuli amewasihi wananchi wa
Rwanda na wanajumuiya ya
Afrika Mashariki kwa ujumla, kushirikiana kibiashara kwa kutumia fursa zilizopo
huku akibainisha kuwa Tanzania
imeanza juhudi za kuimarisha miundombinu yake ya barabara na kujenga reli ya
kati, ambayo tayari washirika 13 wameonesha nia ya kufanikisha ujenzi huo.
Aidha, Rais Magufuli amewaonya
maafisa forodha na vituo vya ukaguzi kuacha mara moja tabia ya ucheleweshaji wa
upitishaji wa mizigo, na amesema serikali imeshaamua kuwa barabara ya Rusumo
hadi Dar es salaam itakuwa na vituo vitatu ambavyo ni Rusahunga, Singida na
Vigwaza ili magari yatumie muda wa siku 3 badala ya kutumia siku zaidi ya 10,
Kwa upande wake Rais Paul Kagame wa
Rwanda ambaye ameongozana na mkewe Mama Janeth Kagame, pamoja na kuishukuru
Japan kwa kufadhili mradi huo amesema Tanzania na Rwanda zina kila sababu ya
kushirikiana kiuchumi na ameongeza kuwa ni matumaini yake kujengwa kituo hicho
kutaongeza biashara na idadi ya watu wanaovuka daraja kutoka 2,000 wa sasa hadi
watu zaidi ya 15,000 kwa siku.
Akiwa Rwanda Rais, Magufuli
amefanya mazungumzo na mwenyeji wake Rais Paul Kagame na hapo Kesho Rais
Magufuli atashiriki maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 22 ya mauaji wa Kimbari
yaliyotokea mwaka 1994 ambapo watu takribani milioni 1,000,000 waliuawa.
Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano,
IKULU
06 April, 2016
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Rais wa Rwanda Mhe. Paul Kagame wakikata utepe kwa pamoja kuashiria uzinduzi rasmi wa daraja la kimataifa la Rusumo, mchana huu. Tukio hilo limehudhuriwa na viongozi wa ngazi za juu serkalini kutoka Nchi zote mbili, Mabalozi, na Viongozi wa Taasisi mbambali za Kitaifa na Kimataifa.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Rais wa Rwanda Mhe. Paul Kagame wakifurahia mara baada ya kuzindua rasmi daraja la kimataifa la Rusumo, mchana huu. Tukio hilo limehudhuriwa na viongozi wa ngazi za juu serikalini kutoka Nchi zote mbili, Mabalozi, na Viongozi wa Taasisi mbambali za Kitaifa na Kimataifa.
Muonekano wa sehemu ya Daraja hilo la Rusumo
Jiwe la msingi lililowekwa baada ya uzinduzi wa daraja hilo
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Rais wa Rwanda Mhe. Paul Kagame wakipita kwenye Daraja hilo la Rusumo mara baada ya uzinduzi
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Rais wa Rwanda Mhe. Paul Kagame wakikata utepe kwa pamoja kuashiria uzinduzi wa Kituo cha Huduma kwa Pamoja Mpakani (OSBP) cha Rusumo. Tukio hilo limehudhuriwa na viongozi wa ngazi za juu serkalini kutoka Nchi zote mbili, Mabalozi, na Viongozi wa Taasisi mbambali za Kitaifa na Kimataifa.
Picha ya pamoja mara baada ya uzinduzi wa huo
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...