Kaimu Meneja wa Idara ya Takwimu za Ajira na Bei wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Bi. Ruth Minja akitoa ufafanuzi kwa wahariri wa vyombo vya Habari kuhusu matokeo ya Utafiti wa Watu wenye uwezo wa kufanya Kazi leo jijini Dar es salaam. Matokeo hayo yataiwezesha Serikali kuangalia upya tija ya utendaji kazi katika shughuli zinazofanywa na makundi mbalimbali ili kubaini mchango wake katika kukuza Pato la Taifa.

Kaimu Meneja wa Idara ya Takwimu za Ajira na Bei wa Ofisi wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Bi. Ruth Minja akitoa ufafanuzi kwa wahariri wa vyombo vya Habari kuhusu matokeo ya Utafiti wa Watu wenye uwezo wa kufanya Kazi. Kushoto kwake ni Hashim Njowele na Saruni Njipay, Watakwimu wa Idara ya Ajira na Bei wa Ofisi hiyo.
Baadhi ya Wahariri na Waandishi wa Habari waliohudhuria ufafanuzi kwa wahariri wa vyombo vya Habari kuhusu matokeo ya Utafiti wa Watu wenye uwezo wa kufanya 2014 Kazi leo jijini Dar es salaam.

Na. Aron Msigwa-Dar es salaam. 
OFISI ya Taifa ya Takwimu (NBS) imesema kuwa takwimu za matokeo ya utafiti wa Watu Wenye Uwezo wa Kufanya Kazi wa Mwaka 2014 zitatumika kufanya maboresho ya Mipango na Sera mbalimbali za kukuza ajira na kupunguza umasikini nchini.

Matokeo ya utafiti huo yameonesha kuwa asilimia 70.9 ya muda wa watu wenye umri wa miaka 15 au zaidi kwa siku hutumika kwenye shughuli zisizo za uzalishaji ikilinganishwa na asilimia 18.5 inayotumika kwenye shughuli za kiuchumi. 

Akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari leo jijini Dar es salaam Kaimu Meneja wa Idara ya Takwimu za Ajira na Bei wa Ofisi hiyo Bi. Ruth Minja amesema kuwa matokeo hayo yataiwezesha Serikali kuangalia upya tija ya utendaji kazi katika shughuli zinazofanywa na makundi mbalimbali ili kubaini mchango wake katika kukuza Pato la Taifa.

Amesema kwa mujibu wa utafiti huo Tanzania ina nguvu kazi ya Taifa ya watu milioni 22.3 wanaume wakiwa milioni 11 na wanawake wakiwa milioni 11.2 huku idadi ya watanzania walio nje ya nguvu kazi ya Taifa wakifikia milioni 3.4.

Amefafanua kuwa idadi ya watanzania walio kwenye ajira ni milioni 20 ikilinganishwa na watu milioni 2.2 ambao hawako kwenye ajira huku akibainisha kwamba kiwango cha nguvu kazi iliyo katika uzalishaji wa bidhaa na huduma za kiuchumi na nguvu kazi iliyo tayari kujihusisha na uzalishaji mali kimepungua kutoka asilimia 89.6 mwaka 2006 hadi asilimia 86.7 ya mwaka 2014.

Kwa mujibu wa utafiti amesema kiwango cha watu wenye umri wa kufanya kazi walio na ajira kwa upande wa wanaume kwa mwaka 2006 kilifikia asilimia 80.8 ikilinganishwa na asilimia 82.1 za mwaka 2014 huku kiwango hicho hicho kwa upande wa wanawake kwa mwaka 2014 kikifikia 73.8 kutoka 77.6 za mwaka 2006.

“ Kiwango cha watu wenye umri wa kufanya kazi walio na ajira kwa ujumla kimepungua, hii inaonesha kuwa, kiwango cha uchumi kuzalisha ajira kimepungua kidogo kutoka asilimia 79.2 mwaka 2006 hadi asilimia 77.8 mwaka 2014” Amesema.

Kuhusu masaa ya kufanya kwa watu wenye umri wa miaka 15 na kuendelea Bi. Ruth Minja amesema kuwa kati ya mwaka 2006 hadi 2014 kumekuwa na ongezeko la masaa ambayo watu hufanya kazi kwa makundi yote ya ajira akifafanua kuwa watu wanaofanya kazi kwa malipo na waliojiajiri wamekuwa wakifanya kazi zaidi ya saa 50 kwa wiki kuliko hali nyingine za ajira.

“ Napenda kuwaeleza kuwa takwimu hizi zitasaidia kuboresha sera ya ajira na programu nyingine ili kuwe na uwiano kati ya saa za watu wanaofanya kazi, uzalishaji na malipo wanayopewa” Amesisitiza.

Aidha, amefafanua kuwa kwa upande wa ukosefu wa ajira kwa muda mrefu kwa watu wenye umri wa miaka 15 au zaidi kote nchini wananwake wana kiwango kikubwa cha ukosefu wa ajira kuliko wanaume kwa miaka yote ya utafiti uliofanywa na Ofisi hiyo toka mwaka 2006 hadi 2014.

Amesisitiza kuwa ipo haja kwa Serikali na wadau mbalimbali kushughulikia kiwango cha watu wasio na kazi na wale ambao hawako tayari kufanya kazi yoyote ya kiuchumi kutokana na ongezeko lake kuwa kubwa kutokana na athari yake kwa uchumi wa taifa. 

“ Kiashiria hiki katika utafiti tulioufanya kinabainisha kuwa kiwango cha watu ambao hawakuwa na kazi wala hawakuwa tayari kufanya kazi yoyote ya kiuchumi kimeongezeka kutoka ailimia 10.4 za mwaka 2006 hadi 17.2 za mwaka 2014 “ Amesisitiza.

Ameeleza kuwa kufuatia kiashiria hicho wanawake wana kiwango kikubwa zaidi kuliko wanaume kwa kuwa wao hujishughulisha na shughuli za nyumbani ambazo sio za kiuchumi zikiwemo za kufua nguo, kupika na malezi ya watoto.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. Hii ni hatua nzuri takwimu zisiachiwe tu kukaa kwenye makabati bila kufanyiwa kazi hasa hizi za ajira ya vijana zinahitaji ufumbuzi kufuatana na maeneo vijana hao walipo.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...