Na Jacquiline Mrisho- MAELEZO
Tanzania imepiga hatua kubwa sana katika sekta ya mawasiliano hadi kufikia kuwa kwenye kundi la nchi zilizoendelea kimawasiliano Duniani.
Takwimu zinaonyesha kuwa watanzania takribani milioni 39 wana laini za simu za kiganjani pamoja na watumiaji wa intaneti takribani milioni 20 ambapo miaka ya nyuma idadi ya laini za simu za kiganjani zilikuwa 2,963,737.
Haya ni maendeleo makubwa yanayoifanya Tanzania kuwa nchi bora kwa upande wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Mhandisi James Kilaba alisikika akisema kwamba,"Ukuaji wa kasi wa sekta ya mawasiliano nchini umechangia sio tu katika kuboresha maisha ya wananchi kijamii na kiuchumi bali unachangia sana katika kuinua pato la Taifa".
Ukuaji huu umetokana na kuwepo kwa sera, sheria, kanuni na mfumo mzuri wa utoaji leseni za huduma za mawasiliano.Kama wasemavyo wahenga kuwa ya Kaisari tumpe Kaisari basi sifa zote ziwaendee Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania kwa kazi nzuri wanazozifanya.
TCRA wana jukumu la kusimamia shughuli hizo zote wakishirikiana na wadau wa mawasiliano nchini katika kusimamia na kuzitekeleza kwa makini sera,sheria na kanuni hizo ili kuwezesha kupatikana kwa huduma za mawasiliano nchini kote kwa kushawishi uwekezaji ,kusimamia vizuri ushindani pamoja na kutoa fursa sawa kwa watoa huduma.
TCRA inaendelea kuhakikisha kuwa rasilimali adimu zikiwemo za masafa na namba za simu zinatumika kwa makini ili kukidhi mahitaji ya Taifa na maendeleo ikiwa ni kutekeleza lengo la Serikali la kuwawezesha wananchi wote kupata habari na kuhakikisha hawaachwi nyuma katika maendeleo ndani ya karne hii ya utandawazi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...