Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Dr. Leonard Masale (katikati) akimkabidhi kombe la ubingwa nahodha wa Barass Sports Centre baada ya timu hiyo kutwaa ubingwa wa Airtel Rising Stars mkoa wa Mwanza juzi. Kushoto ni Meneja wa Airtel Kanda ya Ziwa Ezekiel Nengwa.
Wachezaji wa Barass Sports Centre kabla ya
mchezo wa fainali dhidi ya Hamas ambapo walishinda 6-1 na kutwaa uchampioni wa
Airtel Rising Stars mkoani Mwanza.
TIMU ya wavulana ya Barass
Sports Center imetawazwa kuwa bingwa wa mashindano ya vijana chini ya umri wa
miaka 17 ya Airtel Rising Stars mkoa wa Mwanza baada ya kuiadhibu Hamas Sports
Center 6-1 katika mechi ya fainali iliyofanyika kwenye uwanja wa DIT nje kidogo
ya jiji la Mwanza.
Mechi hiyo ilitanguliwa na
mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu uliozikutanisha timu za Nyamagana United na
HHT ambapo Nyamagana waliibuka na ushindi mwembamba wa 1-0. Goli hilo pekee
lilifungwa na Khalifan Kamanga katika dakika ya 50.
Katika mchezo wa fainali,
Hamas Sports Center ndiyo waliokuwa wa kwanza kupata goli katika dakika ya 10
lililowekwa kimiani na Rogose Albert kwa shuti kali lililomshinda mlinda mlango
wa Barass Sports Center.
Kuona hivyo Barass
walikuja juu na kulisakama lango la wapinzani wao kama nyuki na kufanikiwa
kupata goli la kusawazisha katika dakika ya 13 kupitia kwa Celuha Nehemia
aliyefanya kazi ya ziada kupangua ngome ya Hamas kabla ya kuweka mpira wavuni.
Hamas walifanya mashambuli
ya nguvu kwa nia ya kupata goli linguine lakini juhudi zao hakuzaa matunda na
kujikuta wakifungwa goli la pili. Goli hili lilifunfuwa na mshambuliaji
machachari Frank Osoro katika dakika ya 27.
Alikuwa ni Osoro tena
aliyewainua mashabiki wa Barass Center baada ya kuwatoka walinzi wa Hamas na
kufunga goli la tatu zikiwa zimebakia dakika mbili tu kabla ya kumaliza kipindi
cha kwanza.
Barass walikianza kipindi
cha pili kwa kasi na kufanikiwa kupata goli la nne katika dakika ya 55 kupitia
kwa Maseke Mabigi ambaye alishirikiana vizuri na washambuliaji wenzake na
kuachia shuti iliyojaa wavuni hivyo kuwakatisha tamaa wapinzani wao.
Mabigi ambaye alikuwa
mwiba mkali kwa walinzi wa Hamas alifanikiwa kufunga goli la tano katika dakika
ya 63 kabla ya Deo Martine kuhitimisha karamu hiyo ya magoli kwa kufunga goli
la sita mnamo dakika ya 77.
Mechi za mashindano hiyo
zimewawezesha makocha kuchangua kombaini ya wavulana ambayo itawakilisha mkoa
wa Mwanza katika fainali za Airtel Rising Stars ngazi ya taifa zinazotarajiwa
kufanyika kwenye uwanja wa kumbukumbu ya Karume jijini Dar es Salaam kuanzia
September 6 hadi 11.
Timu zitakazoshiriki
fainali hizo zitatoka Ilala, Kinondoni, Temeke, Zanzibar, Morogoro, Mbeya,
Lindi, Mwanza na Arusha.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...