Idadi ya mauzo katika soko la hisa Dar es salaam (DSE) imekua kwa asilimia 57 na
kufikia shilingi bilioni 3.3 kutoka shilingi bilioni 2.1 wiki iliyopita kutokana na ukubwa
wa idadi ya mauzo.
Katika taarifa iliyotolewa na Afisa Mwandamizi wa Masoko DSE Bi. Mary Kinabo
imesema kuwa idadi ya mauzo hayo yamekua kutokana na kupanda kwa idadi za hisa
zilizouzwa kutoka shilingi milioni 1.6 hadi kufikia shilingi milioni 2.2.
Aidha taarifa hiyo iliongeza kuwa Benki ya CRDB imeendelea kuongoza kwa idadi ya
hisa zilizouzwa na kununuliwa kwa asilimia 49 ikifuatiwa na Soko la hisa DSE ikiwa na
asilimia 43 na ya tatu ni kampuni ya Bia nchini TBL yenye asilimia 4.
Taarifa hiyo iliendelea kueleza kuwa ukubwa wa mtaji wa soko umepanda kwa
asilimia 0.67 na kufikia shilingi trilioni 23.4 kutoka trilioni 23.2 wiki iliyopita na
ukubwa wa mtaji wa makampuni ya ndani umebaki kwa shilingi trilioni 8.4.
Mbali na hayo taarifa hiyo imeeleza kwamba licha ya mauzo kupanda lakini viashiria
vya soko katika sekta ya viwanda vimeshuka kwa alama 19.47 baada ya bei za hisa
kutoka TBL kushuka kwa asilimia 0.66 huku sekta ya huduma za kibenki kupanda kwa
alama 29.89 kutokana na kupanda kwa kaunta ya DSE na NMB.
Aidha taarifa hiyo imeeleza kuwa viashiria vya soko katika sekta ya huduma za
kibiashara wiki hii imebaki kwenye hali yake ya wiki iliyopita baada ya bei za hisa za
Swissport kubaki kwa shilingi elfu 3.543. Na Ally Daud-Maelezo
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...