Inspekta Jenerali wa Polisi IGP Ernest Mangu anatarajia kukabidhiwa uenyekiti wa
Shirikisho la wakuu wa Majeshi ya Polisi kusini mwa Afrika (SARPCCO) katika
mkutano unaotarajiwa kufanyika tarehe 16 Septemba, 2016 jijini Arusha. IGP Mangu
atakabidhiwa uenyekiti huo kutoka kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi wa nchi ya Msumbiji
ambapo atadumu katika nafasi hiyo kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Mkutano huo utatanguliwa na mkutano wa kamati tendaji za SARPCCO amabazo
zitakutana Septemba 14 na 15 mwaka huu ili kuandaa ajenda na mapendekezo ambayo
yatawasilishwa katika mkutano wa wakuu wa Polisi ambao unatarajiwa kufunguliwa na
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Katika mkutano huo mambo mbalimbali ya kukabiliana na uhalifu yatajadiliwa
ikiwemo uhalifu wa kuvuka mipaka, pamoja na kuweka mikakati na maazimio ya
kufanya Oparesheni za pamoja zinazojumuisha nchi zinazounda shirikisho hilo.
Vilevile, mkutano huo utajadili kwa kina utekelezaji wa maazimio mbalimbali kupitia
kamati tendaji za wakurugenzi wa upelelezi, kamati tendaji ya sheria, kamati tendaji ya
mafunzo na kamati tendaji ya mtandao wa Polisi wanawake.
Aidha, suala la michezo baina ya Majeshi ya Polisi kwa nchi wanachama nalo
litajadiliwa katika mkutano huo.
SARPCCO iliundwa mwaka 1995 kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa Majeshi ya
Polisi kwa nchi za kusini mwa Afrika katika kukabiliana na uhalifu. Mpaka hivi sasa
umoja huo unaundwa na Nchi kumi na tano ambazo ni Tanzania, Angola, Botswana,
Malawi, Lesoto, Mauritius, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo(DRC), Msumbiji,
Namibia, Afrika Kusini, Zambia, Zimbabwe, Swaziland, Madagascar na Seychelles.
Imetolewa na:-
Advera John Bulimba – ACP
Msemaji wa Jeshi la Polisi,
Makao Makuu ya Polisi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...