Na Stella Kalinga, Simiyu

Mkoa wa Simiyu unatarajia kuanza kutumia chaki zilizozalishwa na vijana wa Wilaya ya Maswa mkoani humo kuanzia tarehe Mosi Oktoba, 2016.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) kilichofanyika leo katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki Mjini Bariadi.

Mkuu huyo wa Mkoa amesema Mkoa huo unatumia jumla ya shilingi milioni 25 kununua takribani katoni 1200 za chaki( ambazo zinatengenezwanje ya nchi) kwa mwezi katika shule za Msingi na Sekondari, hivyo akawaasa Watanzania kujenga utamaduni wa kupenda na kuthamini vitu vya nchini kwetu ili kuinua uchumi wa Vijana wazalishaji na Taifa kwa ujumla.

“Tuanze kuwafundisha Watanzania kutoka kwenye dhana ya kuwa Chaki ya Kichina ndiyo bora kuliko inayotengenezwa hapa nchini, nahitaji Maafisa Elimu mkae na Walimu Wakuu, Wakuu wa Shule na Waratibu mjadili na muone namna nzuri ya kupata hizo chaki ambazo zitakuwepo katika Banda la Maswa Uwanja wa Sabasaba Mjini Bariadi katika wiki ya vijana na baadaye katika maduka yatakayokuwepo kwenye kila wilaya”, alisema Mtaka.

Mtaka amesema Maafisa Elimu wote wa Wilaya wahakikishe wazabuni wanaopeleka chaki katika Shule za Msingi na Sekondari wananunua chaki zinazozalishwa na Vijana wa Wilaya ya Maswa ambazo zitatambulika kama ‘MASWA CHALKS’, ambapo Vijana wa Maswa watafungua duka kwa kila wilaya hivyo badala ya kuzifuata chaki hizo mahali zinapozalishwa kila wilaya itazipata chaki hizo katika eneo husika

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa amesema Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi , Vijana , Ajira na Wenye Ulemavu , Mhe. Jenista Mhagama atakapokuja katika Uzinduzi wa wiki ya vijana Oktoba 08, 2016 atakwenda kutembelea kiwanda hicho, kujione uzalishaji unavyoendelea na baadaye Mkoa utaomba kibali kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.   John Pombe Joseph Magufuli, kuruhusu Vijana hawa wa Kitanzania kuzalisha bidhaa hii kwa kutumia malighafi kutoka hapa nchini na kuiuza nchi nzima.

Aidha, Mtaka amesema katika Azma ya Mkoa ya kila wilaya kuzalisha bidhaa moja yaani (one distict one product) pamoja na Vijana wa Maswa kuzalisha chaki, Vijana wa Wilaya ya Meatu watakuwa wakisindika maziwa ya ng’ombe kwa kuwa ni Wilaya ya Meatu ndiyo yenye ng’ombe wengi, hivyo kupitia mradi huo wafugaji wa Meatu na Simiyu kwa ujumla watapata soko la maziwa na thamani yake itaongezeka na yatauzwa katika maduka yatakayokuwepo katika kila wilaya.

Amewataka viongozi kuondokana na dhana ya kuwa kupungunza mifugo ndio njia pekee ya kuwakomboa wafugaji na badala yake wawasaidie kupata majawabu ya changamoto zao ikiwa ni pamaja na kuongeza thamani mazao ya mifugo kama maziwa, ngozi na nyama.

Sanjali na hilo Mtaka ameeleza azma ya kuufanya Mkoa wa Simiyu kuwa Mkoa wa mfano wa kuigwa hasa katika utekelezaji wa maagizo ya Viongozi Kitaifa na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015.

Kwa upande wake Naibu ,Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Meatu, Mhe. Luhaga Mpina amepongeza jitihada hizo zinazofanywa na akaahidi kushirikiana na Serikali ya Mkoa katika suala la uanzishwaji wa viwanda vidogo ambapo aliahidi kusaidia Mkoa wa Simiyu upate kiwanda cha kutengeneza mkaa kwa kutumia mimea mingine tofauti na miti ili kulinda na kutunza mazingira.
 Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (katikati) akizungumza na Wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) katika kikao kilichafanyika leo, mjini Bariadi, (Kushoto )Mwenyekiti wa CCM (M), Dkt. Titus Kamani, (kulia) Katibu Tawala Mkoa Simiyu, Jumanne Sagini.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(wa pili kushoto) akiwaonesha wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa gudulia la Maziwa ya Ng’ombe  yaliyotengenezwa na Vijana wa Meatu(MEATU MILK). (Kushoto )Mwenyekiti wa CCM (M), Dkt. Titus Kamani, (kulia) Katibu Tawala Mkoa Simiyu, Jumanne Sagini.
 Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(wa nne kushoto) akiwaonesha wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa sampuli za chaki (MASWA CHALS) zinazozalishwa na Vijana wa Maswa amabazo zinatarajiwa kuanza kuuzwa Oktoba Mosi, 2016.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...