13/09/2016
Serikali imeendelea
kupokea na kuhakiki madai ya watumishi wa umma yanayohusu mshahara na kuyalipa
kadri ya uwezo wake kifedha.
Hayo yamebainishwa na
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
Angellah Kairuki alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Singida Mjini Mhe. Mussa
Sima lililohusu mpango wa Serikali kulipa madeni ya watumishi.
Waziri Kairuki
amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2014/2015 Serikali ililipa madai ya
malimbikizo ya mshahara wa shilingi 56,293,372,627.37 ambapo yalilipwa kwa
watumishi 55,688 waliokuwa na madai yatokanayo na kupandishwa vyeo, ajira mpya
na sababu nyinginezo.
Aidha, Waziri Kairuki
amesema kuwa kwa mwaka 2015/2016 Serikali imeendelea kulipa madai ya
malimbikizo ya mshahara wa watumishi wa umma ambapo hadi kufika mwezi Juni,
2016 watumishi 31,032 walilipwa jumla ya shilingi 28,929,095,373.89.
Pia ameongeza kuwa
madai ya mishahara ya watumishi 7,871 yenye jumla ya shilingi 13,754,462,429.29
yameshahakikiwa na kuingizwa kwenye mfumo wa taarifa za kitumishi za mshahara
yakisubiri kulipwa na madai ya watumishi 8,776 yanaendelea kuhakikiwa ili
yaingizwe kwenye mfumo tayari kwa kulipwa.
Akijibu swali la Mhe.
Zubeda Sakuru (Viti Maalum) lililohusu changamoto ya maslahi kwa watumishi wa
sekta ya afya Waziri Kairuki amesema kuwa Serikali inatambua na kudhamini
mchango unaotolewa na madaktari, matabibu na wauguzi nchini.
Hivyo, Serikali
imeendelea na jitihada za kuboresha mishahara ya watumishi wake mwaka hadi
mwaka ikiwemo ya wataalamu wa sekta hiyo kwa kuzingatia uwezo wa Serikali wa
kulipa.
Waziri Kairuki amesema
kuwa Serikali inaendelea na utafiti wa tathmini ya kazi, punde itakapokamilika
itapanga mishahara na motisha upya kwa watumishi wote wa umma wakiwemo wa sekta
ya afya.
Aidha, amebainisha
kuwa Serikali itaendelea kuboresha maslahi ya watumishi kadri ya uwezo wake wa
kulipa utakavyoimarika ambapo katika shughuli za kila siku madeni huzalishwa
lakini ni azma yake kuhakikisha madeni hayo yanalipwa mara yanapojitokea.
Mbali na hayo, Waziri
Kairuki ametoa wito kwa wataalamu wa afya na watumishi wote kwa ujumla kufanya
kazi kwa bidii na kwa kuzingatia viapo na maadili ya kazi zao.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...