Na Bashir Yakub.
Mtu anapokufa huacha warithi wa namna mbalimbali. Yumkini ndani mwake waweza kuwamo watoto wenye umri mdogo na hata vichaa. Umri mdogo twaweza kuuhesabu kuanzia mwaka 0 mpaka 18. Aidha wakubwa ambao wamezidi miaka 18 hao nafasi yao inajulikana ikiwa marehemu ameacha mali.
Mali zao watakabidhiwa kwa utaratibu maalum ulioratibiwa na sheria. Swali litakuwa kwa watoto wadogo ambao hawawezi kukabidhiwa, tutahitaji kujua sheria inasemaje.
Hapa kuna mazingira ya aina mbili kwanza, ni pale marehemu anapoacha warithi watoto tu na hakuna mkubwa hata mmoja na pili ni pale anapoacha warithi wakubwa na watoto.
Pia kwa ufupi tutaangalia sheria inavyosema kuhusu mali za mrithi ambaye hana akili timamu. Hii nayo tutaangalia mazingira yote, mazingira anapokuwa na warithi wenzake na mazingira anapokuwa mrithi pekee.
1.MTOTO MDOGO.
Sura ya 352 kifungu cha 23 Sheria ya mirathi kinasema kuwa urithi au hati ya kusimamia mirathi haiwezi kutolewa kwa mtoto mdogo.
Tukiachana na hilo tujue kuwa ikiwa mtoto mdogo si mrithi pekee isipokuwa wapo ndugu zake wengine ambao ni warithi basi mmoja wao muadilifu atateuliwa kusimamia mirathi yote ikiwemo ya mtoto mdogo. Msimamizi huyo atakuwa na wajibu wa kuhakikisha anatunza mali ya mtoto/watoto hao mpaka wanakua na kuwa na uwezo wa kutunza mali zao binafsi.
Pili ni pale ambapo mtoto/watoto wadogo ndio warithi pekee wa mali yaani hakuna mkubwa kati yao. Ikiwa hilo litatokea basi mlezi wa watoto anaweza kuomba mahakamani kusimamia mirathi hadi watakapokua.
Taasisi ya udhamini ( trust cooperation) pia yaweza kuomba au kupewa bila kuomba jukumu la kusimamia mali za watoto hadi watakapokua. Hii ni kutoka kifungu cha 22 cha sheria ya mirathi. Yeyote atakayeteuliwa kati yao atakuwa na wajibu mkubwa wa kuhakikisha anatunza mali za watoto kwa kadri mahakama itakavyoelekeza.
Wakati mwingine wanaweza kujitokeza walezi wengi kila mmoja akitaka kusimamia mali za watoto. Ikiwa itakuwa hivyo basi suala hilo litapelekwa mahakamani na mahakama itaamua nani anafaa kusimamia mali hizo kwa kuzingatia zaidi mustakabali wa baadae ya hao watoto.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...