Mnamo
tarehe 04.11.2016 majira ya saa 23:30 usiku huko katika Shule ya
Sekondari Isuto iliyopo Kijiji na Kata ya Isuto, Tarafa ya Isangati, Wilaya ya
Kipolisi Mbalizi, Mkoa wa Mbeya, askari wawili wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya
waliofahamika kwa majina ya 1. H.4925 PC
PETRO OSCAR MAGANA wa Kikosi cha
Kutuliza Ghasia Mkoa wa Mbeya na 2.
J.1422 PC LUKAS JOSEPH NG’WEINA wa
Wilaya ya Kipolisi Mbalizi walituhumiwa kuwafanyia vitendo vibaya kinyume na
maadili wanafunzi wa kike wa kidato cha nne wa Shule hiyo.
Inadaiwa
kuwa, askari hao kwa pamoja wakiwa kwenye ulinzi wa mitihani ya kitaifa ya
kidato cha nne 2016 waliwatoa kwenye Hostel wanafunzi wa kike kwa kile
walichodai kupiga kelele.
Baada
ya kuwatoa wanafunzi hao, waliwapeleka eneo la kufoleni na kuanza kuwapa adhabu
mbalimbali ambazo ni kupiga push up, kuruka kichura, kushika masikio na
kuwachapa viboko sehemu za makalio vitendo vilivyowasababishia maumivu makali
na kupelekea baadhi ya wanafunzi hao wa kike kuondoa na kuelekea nyumbani kwao.
Kufuatia
vitendo hivyo, Mkuu wa Shule hiyo aitwaye ROSE
MZEE DIHEMBE alitoa taarifa kwa uongozi wa Wilaya ambapo taarifa zilifika
kwa uongozi wa Mkoa ambao mara moja walifika eneo la tukio na kuchukua hatua za
awali ikiwemo kusikiliza malalamikio hayo ya tukio na kuwaondoa askari
waliolalamikiwa na mwisho kuchukua hatua za kinidhamu zilizopelekea kufukuzwa kazi
askari hao.
Hata
hivyo, kutokana na vitendo walivyovifanya askari hao wanatarajiwa kufikishwa
mahakamani mara baada ya uchunguzi kukamilika.
WITO:
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Naibu Kamishna wa
Polisi DHAHIRI A. KIDAVASHARI anatoa
wito wananchi waendelee kuliamini Jeshi la Polisi kwamba halitafumbia macho
vitendo vya askari vinavyokwenda kinyume na maadili ya kazi yao. Pia vitendo
vinavyokwenda kinyume na sheria za nchi. Aidha Kamanda KIDAVASHARI anaomba wananchi kuendelea kutoa taarifa ya vitendo
vyote vya uhalifu vinavyotendwa bila kujali vinatendwa na askari au wananchi wa
kawaida ili hatua kali za kisheria ziweze kuchukuliwa.
Imesainiwa na:
[DHAHIRI A.
KIDAVASHARI - DCP]
KAMANDA
WA POLISI MKOA WA MBEYA.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...