Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani
amewahakikishia wananchi wa Wilaya za Kibiti, Rufiji na Mafia kuwa ujenzi wa gati la
kisasa katika eneo la Nyamisati utaanza wakati wowote baadaye mwakani na
kukamilika ifikapo Machi 2018.
Akizungumza mara baada ya kukagua eneo litakapojengwa gati hilo katika pwani ya
Nyamisati wilayani Kibiti Eng.Ngonyani amewataka viongozi na wananchi wa wilaya
hizo kuwa na uvumilivu katika kipindi hiki ambacho Serikali inatafuta ufumbuzi wa
kudumu.
“Endeleeni kutunza mazingira ya eneo hili na kutunza mazingira ya bahari ili kudhibiti
mabadiliko ya tabia nchi katika eneo lenu, Serikali imejipanga kukabiliana na
changamoto inayowakabili sasa hivyo toeni ushirikiano unaohitajika ili kuiwezesha
Mamlaka ya Bandari nchini(TPA) kutekeleza ujenzi wa gati hili”. Amesisitiza Eng.
Ngonyani.
Naye Mbunge wa Mafia Mhe. Mbaraka Dau amemhakikishia Naibu Waziri Ngonyani
kuwa kukamilika kwa gati la kisasa katika pwani ya Nyamisati kutahuisha shughuli za
kiuchumi kwa wakazi wa Mafia na Mkoa wa pwani kwa ujumla.
“Kukamilika kwa gati hili kutavutia wasafirishaji wengine kuleta vyombo vya usafiri na
hivyo kushusha gharama za usafiri kati ya Kibiti na Mafia ambapo sasa ni zaidi ya
shilingi elfu kumi na tatu kwa safari”. Amesema Mhe. Dau.
Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ngonyani amekagua barabara ya Ikwiriri-Lindi,
Nanyumbu –Masugulu-Mtambaswala na Mangaka -Tunduru na kumtaka Meneja wa
Wakala wa barabara Mkoa wa Mtwara Eng.Dotto Chacha kuhakikisha barabara
inakuwa salama wakati wote kwa kudhibiti madereva wanaoegesha magari barabarani
isivyostahili.
Naibu Waziri Ngonyani yupo katika ziara ya kukagua Miundombinu ya barabara,
Bandari na Mawasiliano katika mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng.Edwin Ngonyani (wa kwanza
kushoto) akitoa maelekezo kwa kaimu Meneja wa Wakala wa barabara (TANROADS)
Mkoa wa Mtwara Eng. Dotto Chacha alipokagua barabara ya Mangaka-Mtambaswala
na Mangaka –Tunduru.
Kaimu Meneja wa Wakala wa barabara (TANROADS) Mkoa wa Mtwara Eng. Dotto
Chacha akimuonesha Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng.Edwin
Ngonyani (katikati) eneo la mzunguko wa Mangaka linalohitaji marekebisho katika
barabara ya Mangaka –Mtambaswala na Mangaka –Tunduru ambao ujenzi wake kwa
kiwango cha lami umekamilika.
Muonekano wa barabara ya Mangaka-Mtambaswala inayounganisha Tanzania na
Msumbiji ambayo ujenzi wake kwa kiwango cha lami umekamilika barabara hii
inatarajiwa kuchochea uchumi wa mkoa wa Mtwara.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...