Na Dotto Mwaibale
WAZIRI
wa Fedha Dk. Philip Mpango anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika
Maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika yatakayofanyika Ukumbi wa
Makumbusho ya Taifa mkabala na Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM)
Maadhimisho
hayo yatafanyika kesho kuanzia saa tatu asubuhi ambapo wadau mbalimbali
wa masuala ya takwimu na wananchi watahudhuria.
Akizungumza
katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo asubuhi Meneja
wa Idara ya Pato la Taifa kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Daniel
Masolwa alisema maadhimisho hayo ni muhimu sana na kuwa kauli mbiu yake
ya mwaka huu ni " Kuimarisha Takwimu za Kiuchumi kwa Mtangamano wa
Kikanda, Mabadiliko ya Miundo na Maendeleo Endelevu"
Masolwa
alisema lengo kuu la kuadhimisha siku hiyo ni kuongeza uelewa mpana
kwa watumiaji wote wa Takwimu Afrika kuhusu umuhimu wa takwimu katika
kupanga mipango ya maendeleo katika sekta zote za kijamii na kiuchumi
katika Bara la Afrika.
Aidha
alisema ni siku ambayo hutoa fursa kwa nchi kutathmini na kufuatilia
malengo yaliyofikiwa katika Mipango ya Maendeleo ya ndani na nje ya
Nchi.
Alisema
Maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika huwa yanaandaliwa na kauli mbiu
mbalimbali kila mwaka zinahusiana na umuhimu wa takwimu katika kupanga
maendeleo na kutunga sera katika Bara la Afrika.
Masolwa
alisema umuhimu wa kuboresha na kuimarisha takwimu za kiuchumi na zenye
ubora kwa utangamano wa kikanda barani Afrika utasaidia kuleta
mabadiliko ya kiuchumi na kufanikisha malengo endelevu, Agenda 2063 ya
Afrika na mipango ya kitaifa ya kukuza uchumi.
Meneja wa Idara ya Pato la Taifa kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Daniel Masolwa (kushoto), akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, kuhusu maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika yatakayofanyika kesho Ukumbi wa Makumbusho ya Taifa mkabala na Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM). Kulia ni Ofisa Habari wa Idara Habari Maelezo, Beatrice Lyimo.
Mkutano na wanahabari ukiendelea.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...