Wajumbe wa Kamati ya Mfuko wa Jimbo la Musoma Vijijini wameagizwa kuhakikisha wanakagua utekelezaji wa miradi ya kilimo ya vikundi vilivyokabidhiwa vifaa kutoka kwenye mfuko huo ili kujiridhisha.

Agizo hilo limetolewa hivi karibuni na Mbunge wa Jimbo hilo, Profesa Sospeter Muhongo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati husika wakati wa mkutano wa hadhara wa kuainisha matumizi ya fedha za Mfuko wa Jimbo kwa Awamu ya Pili uliofanyika katika kijiji cha Tegeruka, Musoma Vijijini.

Ilielezwa kwamba Awamu ya kwanza ya fedha zilizotolewa kwa ajili ya Mfuko wa Jimbo hilo ni shilingi milioni 70,820,000 ambazo zilitumika kwa matumizi mbalimbali ikiwemo shilingi milioni 20,000,000 kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Murangi.

Fedha zingine ni milioni 27,500,000 ambazo zilitumika kwa ajili ya kurekebisha nyumba na madarasa yaliyokuwa yameezuliwa na upepo kwa shule mbili za msingi, milioni 22,500,000 ilitumika kununulia mashine za umwagiliaji, mbegu za mbogamboga na matunda pamoja na dawa za kilimo na shilingi 820,000 zilitengwa kwa ajili ya kuwezesha ufuatiliaji.

Profesa Muhongo alisema ni jukumu la Kamati husika kuhakikisha fedha imetumika kwa matumizi yaliyokubaliwa na aliagiza vikundi vyenye miradi ya kilimo ambayo haijaanza vinyang’anywe vifaa vilivyokabidhiwa na vipewe vikundi vingine vyenye vyenye nia dhabiti ya kuendeleza kilomo.

“Tembeleeni hivi vikundi, mkikuta havijaanza kutumia vifaa tulivyowapatia mvinyanga’anye na vifaa hivyo vigawiwe kwenye vikundi vyenye nia ya dhati,” aliagiza Profesa Muhongo.Akizungumzia Awamu ya Pili ya Mfuko wa Jimbo, Profesa Muhongo alisema Mfuko wa Jimbo umepokea kiasi cha shilingi milioni 38,479,000 ambazo alisema Kamati husika kwa kushirikiana na wananchi pamoja na madiwani wamependekeza zitumike kwa ajili ya kuboresha kilimo.

Alisema shilingi milioni 16,000,000 zitatumika kwa ajili ya kununulia mbegu za kisasa za mihogo za mkombozi kiasi cha vipando 532,000 ambazo zitagawiwa kwenye Kata 21 kwa ajili ya vijiji 68, na shilingi milioni 21,900,000 itatumika kununulia mashine 21 za kukamulia alizeti. 

Aliongeza kuwa hapo awali alisambaza mbegu za alizeti za majaribio kiasi cha kilo 4000 ambazo alisema zimeonesha mafanikio na hivyo aliongeza mbegu zilizoboreshwa kutoka Arusha kiasi cha kilo 5000 ambazo pia zilisambazwa.

Alisema ili kujiongezea kipato kutokana na kilimo cha alizeti, wameamua badala ya kuuza mbegu, wakulima hao watauza mafuta na ndiyo sababu ya kutenga kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya mashine hizo ambazo alizielezea kuwa ni za kuzungusha kwa mikono na hazihitaji mafuta wala umeme.

“Hizi nilitoa fedha yangu na sio katika mfuko wa jimbo; na kukitokea mapungufu nifahamisheni nijazilizie,” alisema.Akizungumzia utaratibu wa mashine hizo, alisema kila Kata itakabidhiwa mashine yake na kwamba zitafungwa kwenye ofisi za kata chini ya usimamizi wa Afisa kilimo.
Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akizungumza jambo wakati wa mkutano wa kujadili matumizi ya fedha za Mfuko wa Jimbo. Kushoto ni wajumbe wa Kamati ya Mfuko wa Jimbo la Musoma Vijijini.
Baadhi ya wananchi wa Kata ya Tegeruka, Musoma Vijijini waliohudhuria mkutano wa kujadili matumizi ya fedha za Mfuko wa Jimbo hilo.
Katibu wa Mfuko wa Jimbo la Musoma Vijijini na Afisa Mipango wa Wilaya ya Musoma, Mukama Rugina (aliyesimama) akizungumza wakati wa mkutano wa kujadili matumizi ya fedha za mfuko huo.
Diwani wa Kata ya Tegeruka, Benjamin Maheke (aliyesimama) akizungumza wakati wa mkutano wa kujadili matumizi ya fedha za mfuko wa Jimbo la Musoma Vijijini.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...