WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wananchi kuacha tabia ya kuhifadhi fedha nyingi majumbani na badala yake wajenge utamaduni wa kuzipeleka benki kuepusha kuhatarisha usalama wao. 

Ametoa ushauri huo jana (Jumatatu, Desemba 5, 2016) wakati akifungua tawi la benki ya Biashara ya Uchumi lililopo wilayani Karatu mkoani Arusha akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani hapa.

Alisema tabia ya baadhi ya wananchi kuhifadhi kiasi kikubwa cha fedha majumbani si nzuri kwa sababu wanahatarisha usalama wao, hivyo ni vyema wakatumia benki mbalimbali zilizoko kwenye maeneo yao kwa ajili ya kutunza fedha zao.Akizungumzia kuhusu kufunguliwa kwa tawi la benki ya Uchumi wilayani Karatu, Waziri Mkuu alisema unaashiria ukuaji wa uchumi wa wilaya hiyo kwa kuwa benki ni kichocheo cha maendeleo.

Katika hatua nyingine Waziri Mkuu aliushauri uongozi wa benki ya Uchumi kuangalia uwezekano wa kupunguza kiasi cha riba wanachokitoza katika mikopo wanayoitoa ili kuwawezesha wananchi kukopa na kupata tija.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa benki hiyo Bw. Wilson Ndesanjo alisema benki hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya mtaji mdogo jambo linalowasababisha washindwe kufungua matawi katika mikoa mingine.

“Changamoto nyingine ni baadhi ya wateja kushindwa kurejesha mikopo kwa wakati, ambapo hatua za kisheria zikichukuliwa wanakimbilia mahakamani. Matukio haya yanadhoofisha kasi ya utoaji wa huduma kwani kesi zinachukua muda mrefu,” alisema.

Bw. Ndesanjo alisema kuna baadhi ya kesi zimechukua miaka sita bila ya kumalizika hivyo kuzuia fedha ambazo kama zingerejeshwa kwa wakati zingezungushwa kwa wananchi wengine.

Benki ya Uchumi ilianzishwa Septemba 22, 2005 ikiwa na mtaji wa sh. milioni 372. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Oktoba, 2016 mtaji huo umefikia sh. bilioni 5.4 hivyo umeongezeka mara 14.5 zaidi ya ule wa awali uliokuwepo wakati wa uanzishwaji wake.


IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU

JUMANNE, DESEMBA 6, 2016.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...