Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Dkt. Mussa Iddi Mgwatu leo
amefungua mafunzo elekezi kwa mameneja wa mikoa na vituo vya TEMESA juu ya
tozo za matengenezo ya magari, pikipiki na mitambo pamoja na uaandaji wa taarifa
za uzalishaji za mwezi kwa watumishi wa TEMESA kutoka katika mikoa na vituo mbali
mbali vilivyopo nchini.
Katika hotuba yake Dkt. Mgwatu amewataka watumishi hao kuhakikisha kuwa
wanashiriki mafunzo hayo kwa umakini mkubwa ili kuleta mabadiliko chanya kwa
TEMESA na kuondoa kero mbalimbali zilizopo sasa, ikiwemo kero ya gharama kubwa za
matengenezo ya magari, pikipiki na mitambo ya serikali na kuwataka watumishi hao
kuondokana na wazabuni wanaouza vipuri na vilainishi vya magari kwa bei ghali isiyo
ya soko.
“Mafunzo haya ni gharama na kwa hiyo haitakuwa jambo jema tukarudi katika vituo
vyetu na kuendeleza mambo yale yale kwa mazoea. Tutakuwa hatujatenda haki kwa
wananchi na kwa taifa kwa ujumla. Niwe mkweli kuwa nitachukua hatua kali pale
nitakapoona mkoa au kituo hakifanyi vyema katika utendaji kazi wake” alisema Dr.
Mgwatu.
Nae Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Matengenezo Mhandisi Sylvester Semfukwe
amesema kuwa idara yake imeandaa mada mbali mbali kwa ajili ya mafunzo hayo
zikiwemo: Tozo ya matengenezo ya magari, pikipiki na mitambo kwa kuzingatia muda
halisi wa matengenezo, Mfumo mpya wa kuandaa taarifa za uzalishaji za kila mwezi,
Namna ya kubaini vipuri bandia kwa njia ya kielektroniki, Masuala ya masoko na
huduma kwa mteja pamoja na mwongozo wa uwandaaji wa bajeti ya mwaka wa fedha
2017/18.
Mafunzo hayo ya siku tano yaliyoanza jana katika Ukumbi wa TBA mkoani Dodoma,
yanashirikisha jumla ya mikoa 19 yenye vituo vya TEMESA, yanatarajia kukamilika
Ijumaa tarehe 20/01/2017. Aidha mafunzo hayo ni muendelezo wa mafunzo kama
hayo yaliyofanyika mwezi Desemba, 2016 mkoani Dar es Salaam na yalishirikisha
mikoa sita.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Dkt. Mussa Iddi
Mgwatu (aliesimama) akifungua mafunzo elekezi juu ya tozo za matengenezo
ya magari, pikipiki na mitambo kwa watumishi wa TEMESA kutoka mikoa 19.
Kushoto kwake ni Mkurugenzi wa Uzalishaji na Matengenezo Mhandisi Sylvester
Semfukwe na kulia ni Meneja wa TEMESA Dodoma. Mafunzo hayo ya siku 5
yanafanyika Mkoani Dodoma katika ukumbi wa TBA.
Washiriki wa mafunzo elekezi juu ya tozo za matengenezo ya magari, pikipiki
na mitambo yanayofanyika Mkoani Dodoma katika ukumbi wa TBA wakisikiliza
hotuba ya Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Dkt.
Mussa Iddi Mgwatu (hayupo pichani). Mafunzo hayo ya siku tano yanashirikisha
watumishi wa TEMESA kutoka mikoa 19.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo elekezi juu ya tozo za matengenezo ya magari,
pikipiki na mitambo yanayofanyika mkoani Dodoma katika ukumbi wa TBA
wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na
Umeme (TEMESA), Dkt. Mussa Iddi Mgwatu (alieketi katikati) baada ya ufunguzi.
Mafunzo hayo ya siku tano yanashirikisha watumishi wa TEMESA kutoka mikoa
19.
Mameneja kutoka mikoa 19 yenye vituo vya Wakala wa Ufundi na Umeme
(TEMESA) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu wa TEMESA Dkt.
Mussa Iddi Mgwatu (alieketi katikati) baada ya ufunguzi wa mafunzo elekezi juu
ya tozo za matengenezo ya magari, pikipiki na mitambo yanayoendelea mkoani
Dodoma katika ukumbi wa TBA.
Picha zote na Theresia Mwami, TEMESA.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...