NA VICTOR MASANGU, KIBITI
KATIKA kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano katika kupambana na wimbi la umasikini hususan kwa vijana na wakinamama, halmashauri ya Wilaya mpya ya Kibiti mkoani Pwani imejiwekea mipango madhubuti kwa ajili ya kuweza kuwasaidia katika vikundi vya ujasiriamali kwa lengo la kuweza kuondokana na dhana ya kuwa tegemezi na badala yake wafanye kazi ili kuweza kuleta maendeleo.
Hayo yalibainishwa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Kibiti, Alvera Ndabagoyo wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi katika mahojiano maalumu kuhusiana na changamoto ya siku nyingi ya wimbi la umasikini kwa vijana wa wakinamama pamoja na mikakati yao waliyojiwekea ili kuondokana kabisa na hali hiyo.
Mkurugenzi huyo alisema kwamba kwa sasa anatambua kuna baadhi ya vijana na wakinamama katika Wilaya hiyo ya Kibiti wanakabiliwa na tatizo la kutokuwa na ajira hivyo uongozi wa halmashauri hiyo umeshaanza kufanya jitihada za hali na mali katika kuhakikisha fedha ambazo zitakuwa zikitengwa kwa ajili yao zinawafikiwa walengwa ili waweze kuzifanyia shughuli halali za kimaendeleo na kujipatia kipato.
Pia Alvera alibainisha kuwa katika mwongozo wa serikali inatakiwa kila halmashauri katika kila bajeti yake ya mwaka itenge kiwango cha asilimia 10 cha fedha kwa ajili ya kuweza kuvisaidia vikundi mbali mbali vya wakinamama pamoja na vijana ili waweze kuendelea kufanya shughuli zao mbali mbali za kijasiriamali lengo ikiwa ni kuweza kupamabana na umasikini.
Aidha aliongeza kuwa ana imani kubwa endapo vikundi vya vijana na wakinamama katika Wilaya ya Kibiti vikijiunga kwa pamoja na kuwezeshwa kwa kupatiwa fedha kwa ajili ya kufanyia biashara vitaweza kufika mbali na kuweza kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo kuanzia ngazi za familia zao hadi kuwasaidia na wananchi wengine .
Katika hatua ngingine Mkurugenzi huyo alitoa wito kwa wananchi wote wa Wilaya ya Kibiti kuachana na kuwa na tabia ya kuwa tegemezi kila kukicha na badala yake sasa wabadilike na kujiunga katika vikundi mbai mbali vya ujasiliamari ili pindi fedha inapotolewa na halmahsuari iwe rahisi kuwafikia walengwa kuliko kuwa mtu mmoja mmoja.
Hata hivyo Mkurugenzi huyo aliahidi kushirikiana bega kwa began a baraza la madiwani, watendaji, pamoja na wadau wa maendeleo katika kuhakikishwa wanapambana vilivyo katika kuzitatua kero na changamoto mbali mbali ambazo zimekuwa zikiwakabili kwa kipindi kirefu wananchi wa Wilaya mpya ya Kibiti mkoani Pwani.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...