Na Lydia Churi-Mahakama
Mahakama ya Tanzania inatarajia kukamilisha miradi ya ukarabati na ujenzi wa
majengo 70 ya Mahakama katika kipindi cha miaka miwili ili kusogeza karibu huduma
ya utoaji haki kwa wananchi.
Ili kusogeza huduma hiyo kwa wananchi, majengo ya Mahakama kuu katika mikoa tisa
yanatarajiwa kukamilika katika kipindi cha miaka miwili, Mahakama za Mikoa sita
zitajengwa ndani ya miezi 6-12 wakati Mahakama za Wilaya 19 na za Mwanzo 36
zinatarajiwa kukamilika ifikapo Desemba 2017.
Akizungumza wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika hivi
karibuni, Kaimu Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Juma alisema Mahakama
kwa kushirikiana na Wakala wa Majengo (TBA), Chuo Kikuu cha Ardhi, Baraza la Ujenzi
la Taifa, Benki ya Dunia na wadau wengine wanaendeleza na kukamilisha miradi ya
ujenzi wa Mahakama Kuu katika mikoa tisa nchini.
Aliitaja mikoa ambayo majengo ya Mahakama Kuu yatafanyiwa ukarabati na mengine
kujengwa ndani ya kipindi cha miezi 24 kuwa ni Mbeya, Kigoma, Mara, Tanga na Dar
es salaam. Mikoa mingine ni Arusha, Morogoro, Mwanza na Dodoma.
Alisema nia ya Mahakama ni kuwa na Mahakama Kuu katika kila Mkoa ili kusogeza
huduma za Mahakama kwa wananchi.
“Tunapaswa kuwa na Mahakama Kuu 26 kwenye kila ngazi ya Mkoa, kwa sasa tunazo
Mahakama Kuu kwenye kanda 14 tu”, alisema Kaimu Jaji Mkuu.
Aidha, mikoa 12 isiyokuwa na Mahakama Kuu ni pamoja na Songwe, Katavi, Njombe,
Lindi, Kigoma na Mara. Mikoa mingine ni Singida, Morogoro, Pwani, Simiyu, Geita na
Manyara.
Kaimu Jaji Mkuu alisema kuwa wakati huo huo, Mahakama ya Tanzania inatarajia
kukamilisha ujenzi wa Mahakama za Hakimu Mkazi katika mikoa sita ya Manyara,
Geita, Simiyu, Njombe, Katavi na Lindi katika kipindi cha kati ya miezi 6 na mwaka
mmoja.
Kwa upande wa Mahakama za Wilaya na zile za Mwanzo, Kaimu Jaji Mkuu alisema
wanakusudia kujenga Mahakama za Wilaya 19 na za Mwanzo 36 ambazo zitakamilika
ifikapo Desemba 2017.
Alisema hatua hii ya ujenzi wa Mahakama hizi si tu kwamba itasogeza karibu huduma
za Mahakama kwa wananchi bali pia italeta mabadiliko makubwa ya miundombinu ya
mahakama na kuweka historia ya upatikana wa miundombinu kwa wingi na kwa kifundi
kifupi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...