Serikali imewataka wanufaika wa ruzuku ambao hawakuitumia kama ilivyokusudiwa warejeshe fedha walizopatiwa mara moja na vyombo vya ulinzi na usalama vihakikishe waliohusika kuidhinisha wanawajibishwa. Agizo hilo limetolewa Desemba, 12, 2017 na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo Mkoani Singida wakati wa ziara yake ya kutembelea Migodi ya Dhahabu kwa ajili ya kujionea shughuli zinazoendelea na kuzungumza na wachimbaji.

“Aliyenufaika na ruzuku na hakufanya lolote, arejeshe mara moja fedha hiyo na aliyehusika kuwapatia ruzuku watu hawa hali yakuwa anaelewa hawakuwa na dhamira ya kuendeleza uchimbaji nae achukuliwe hatua,” aliagiza Nyongo.
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (kushoto aliyenyoosha mkono) akielekeza jambo alipotembelea Mgodi wa Dhahabu wa Mwandami Small Scale Mine uliopo katika Kijiji cha Sambaru, Kata ya Mang’onyi Wilayani Ikungi. 

Agizo hilo linafuatia malalamiko ya wachimbaji wadogo ambao hawakunufaika na mpango huo wa ruzuku ambapo walimueleza kwamba wapo baadhi ya watu wasiostahili lakini walipatiwa ruzuku. Naibu Waziri Nyongo alisema anampongeza Rais John Magufuli kwa uamuzi wake wa kusimamisha utoaji wa ruzuku kwani imeshindwa kufikia matarajio yaliyokusudiwa. Alisema Serikali ilisimamisha utoaji wa ruzuku kwa wachimbaji wadogo wa madini nchini baada ya kubaini kwamba imeshindwa kuleta mafanikio yaliyokusudiwa.

Nyongo alisema dhamira ya Serikali ya kutoa ruzuku ilikuwa ni kuhakikisha wachimbaji wadogo wa madini nchini wanaweza kuendeleza machimbo yao kwa kufanya shughuli zenye tija kwao na Taifa kwa ujumla. Hata hivyo alisema dhamira hiyo haikuzaa matunda yaliyokuwa yamekusudiwa kwani imedhihirika kwamba ruzuku iliyotolewa haikuwanufaisha walengwa kama ilivyotarajiwa badala yake ilinufaisha watu wachache tofauti na ulivyokuwa mpango mzima wa utoaji wake.
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (kushoto) akitazama mtambo wa kusaga mawe yenye Madini ya Dhahabu uliopo kwenye Mgodi wa Mzaki na Wenzake uliopo katika Kijiji cha Mwau, Wilayani Ikungi. Kulia ni Mmoja wa Wamiliki wa mgodi huo, Kasirate Mzaki. 

“Wapo wachimbaji wachache ambao walifanikiwa kupata ruzuku na waliweza kuendeleza migodi; japo hawa ni wachache tofauti na malengo ya Serikali,” alisema Naibu Waziri Nyongo. Mbali na hilo, alisema baadhi ya wachimbaji wadogo walipewa ruzuku na walichimba lakini hawakufanikiwa kwani walichimba kwa kubahatisha bila kuwa na elimu ya kutosha ya kutambua uwepo wa mashapo katika maeneo yao.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...