Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akiongozana na Balozi wa Tanzania, nchini Misri, Balozi Mohammed Hamza, wakati wakitoka kwenye Boti baada ya kuhudhuria hafla ya uzinduzi wa Mfereji mpya wa Suez Canal, kwa ajili ya meli za mizigo. Hafla hiyo ilifanyika jana Agosti 6, 2015 jijini.
 Picha na OMR

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mohammed Gharib Bilal jana ameiwakilisha Tanzania katika uzinduzi wa mfereji mpya wa Suez unaounganisha mabara ya Ulaya, Afrika na Asia. Mfereji huu mpya ambao Misri inauita "zawadi mpya kwa Dunia" unalenga kukuza uchumi katika usafiri wa maji na utarahisisha usafirishaji wa mizigo kwa mabara haya matatu, huku Misri ambayo kijiografia iko jangwani ikitegemea kukuza uchumi wake kutokana na meli zitakazopita katika mfereji huo.

Mradi wa ujenzi wa Mfereji huu mpya umejengwa kwa mwaka mmoja licha ya kupangwa kukamilika baada ya miaka mitatu na umetumia kiasi cha dola za Marekani Bilioni Nane ambazo zimechangwa kwa njia ya Hisa na wananchi wa Misri kwa kipindi kisichozidi siku tisa. Mfereji huu ambao umezinduliwa jana, unatoa fursa kwa Meli kupita bila usumbufu tofauti na zamani ambapo ilipaswa Meli kusimama ili kupishana lakini sasa kila upande wa Meli utapita bila kuathiri upande mwingine.

Sherehe hizo za aina yake zimehudhuriwa na viongozi kadhaa wa nchi mbalimbali na kupata kuripotiwa na vyombo vyote vikubwa duniani na hivyo kutoa picha ya kuwa Afrika inapiga hatua katika kukuza uchumi wake pamoja na kuonesha dunia kuwa fursa mpya za maendeleo zipo Afrika.

Sherehe hizo za  aina yake zilipambwa na maonesho ya ndege za kivita zilizotanda anga la Mfereji mpya wa Suez huku zingine zikiruka kwa kasi na kutoa moshi ulioakisi bendera ya Misri, zingine zikipeperusha bendera ya nchi hiyo.

Katika tukio hilo la kuathimisha tukio hilo la kihistoria   serikali ya Misri ilitangaza kuwa  siku hiyo ni ya mapumziko huku ulinzi mkali ukiimarishwa katika miji yote mikuu ya nchi hiyo huku jiji la Cairo walipofikia  viongozi mbalimbali wa kimataifa likiwa chini ya uangalizi wa kijeshi kwenye maoneo yote muhimu. Barabara ya kwenda eneo la Islamelia zilikofanyika sherehe hizo ilifungwa kwa siku nzima,  walioruhusiwa kupita  ni viongiozi na wageni mbalimbali  waalikwa waliotakiwa kuhudhuria tukio hilo la kihistoria.

 Rais wa Misri Abdel  Fatah  Sisi alisema kufunguliwa kwa Mfereji  ni uthibitisho kwamba Misri inaweza na kueleza kwamba njia hiyo itaimarisha zaidi shughuli za usafirisha na kufungua fursa zaidi kwa mataifa  duniani.

Katika moja ya matukio ya  uzinduzi huo Rais Fatah na viongozi mbalimbali waliohudhuria sherehe hizo walisafiri katika meli za kifahari huku kiongozi huyo wa Misri akivalia mavazi maalumu ya kijeshi akiwa juu ya sehemu ya uwazi wa meli hiyo pamoja na kijana mdogo mwanafunzi wa miaka tisa aliyevalia kijeshi na kupeperusha bendera ya  Misri kama ishara ya kufunguliwa rasmi kwa mfereji huo.

Shughuli  ilimazika usiku  kwa  maonesho mbalimbali ya sanaa na utamaduni wa Misri  na kuhudhuriwa na viongozi na wageni wote waalikwa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...