WANANCHI zaidi ya 265 wa mtaa wa Upendo, Mbezi Salasala wilayani Kinondoni wamelishukuru Shirika
la Majisafi na Majitaka Dar es salaam (DAWASCO), kwa kuwafikishia huduma ya Majisafi waliyoipatia
shida kwa zaidi ya miaka 10 iliyopita.
Akizungumza wakati wa mkutano wa pamoja wa serikali za mitaa na DAWASCO, Mjumbe wa mtaa wa
Upendo Bw. Robert Massawe amepongeza juhudi zilizofanywa na Dawasco za kuwapatia huduma ya Maji
wananchi wa eneo lake na kwamba juhudi hizo zinaendana na kauli ya serikali ya awamu ya tano
inayosema hapa kazi tu.
Akieleza historia fupi ya eneo hilo Bw. Massawe alisema tangu watu waanze kuhamia eneo hilo huduma ya
Maji ilikuwa ni ya kununua kutoka mtaa mwingine wa mbali ambao ulikuwa umefikiwa na huduma hiyo ya
Maji.
“Ilifikia kipindi gharama ya kununua Maji ni kubwa kuliko gharama ya chakula, na wananchi wengi walikuwa
wakitumia muda wao mwingi kuhangaika kutafuta Maji jambo ambalo lilikuwa likikwamisha kutekeleza
majukumu mengine ya kujenga nchi” alisema Massawe.
Nae mmoja wa wakazi wa eneo hilo, Bi. Sofia alisema; “Kweli DAWASCO imemtua mama ndoo ya Maji
kichwani, sisi akina mama ndio tuliokuwa tukiteseka zaidi na suala la Maji, lakini akina mama wa mtaa huu
tulijitoa ili kupambana na janga la Maji ambalo lilikuwa likitukabili, na hatimaye tumefanikiwa kupata
huduma ya Maji”
Kwa upande wa Dawasco, Meneja wa Mkoa wa Tegeta, Bw. Alpha Ambokile amewataka wakazi wa mtaa
huo kujitokeza kwa wingi kufanya maombi ya kuungiwa huduma ya Maji kwa kuwa tayari huduma hiyo
imefika katika makazi yao, baada ya kuhangaika kwa muda mrefu wakisaka huduma hiyo, na ameahidi
kuwaunganishia huduma Maji mapema na kwa uharaka zaidi, mara tu baada ya kupokea maombi yao ya
kuungiwa huduma.
“Ninawaomba mjitokeze kwa wingi ili kwa pamoja tuweze kuwaunganishia huduma ya Maji, nitawatengea
siku yenu maalum ambayo timu yangu ya ufundi itakuja kuwafanyia maunganisho ya Maji, ambao bado
hamjafanya maombi, fanyeni haraka ili tuweze kuwaunganishia wote kwa pamoja huduma ya Maji” alisema
Ambokile.
Sehemu ya wakazi wa mtaa wa Upendo, Mbezi salasala wakiwa na Mjumbe wa mtaa huo, Bw. Robert
Massawe (aliyevaa shati ya bluu), wakisikiliza kwa makini katika kikao cha pamoja na uongozi wa Shirika la
Maji safi na Majitaka Dar es salaam (DAWASCO) kutoka mkoa wa Tegeta, baada ya mtaa huo kufikiwa na
huduma ya Majisafi na salama kwa mara ya kwanza tangu waanze kuhamia katika makazi hayo, jijini Dar
es salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...