Waziri wa Mafuta wa Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, Mhe. Aime Ngoi-Mukena Lusa- Diese amesema Serikali ya Kongo iko tayari kushirikiana na serikali ya Tanzania kwenye Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki.
Mhe Lusa- Diese aliyasema hayo katika kikao kilichokutanisha ujumbe wake na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini pamoja na taasisi zake kilichofanyika jijini Dar es Salaam. 

Alisema kuwa lengo la ziara yake lilikuwa ni Serikali ya Kongo kuomba kushiriki na kuwa sehemu ya mradi wa bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki linalojengwa kutoka Hoima nchini Uganda hadi Tanga nchini Tanzania kutokana na kwamba sehemu ya Kongo ina mafuta. 
Alisema kuwa nchi ya Kongo kupitia wataalam wake ipo tayari kushirikiana na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Nishati na Madini ili kufanikisha mradi mkubwa wa bomba la mafuta ambalo litanufaisha nchi zote za Afrika Mashariki. 
Naye Mkurugenzi kutoka Kampuni ya Oil of DR Kongo kutoka Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, Giuseppe Ciccarelli alisema kampuni yake ina uzoefu kwenye utafiti na uchimbaji wa mafuta na kusisitiza kuwa mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki, kampuni yake itakuwa na uwezo wa kusafirisha kuanzia mapipa 30,000 hadi 100,000 kwa siku kulingana na mahitaji. 
Aliishukuru serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Nishati na Madini kwa kuwa tayari kushirikiana na Kongo kwenye mradi wa bomba la mafuta na kuongeza kuwa kupitia mradi huu nchi zote kwa pamoja zitapata mapato na kukua kwa uchumi wake. 
Awali akizungumza katika kikao hicho, Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo alisema kuwa Serikali ipo tayari kushirikiana na Kongo katika mradi wa bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki na kuelekeza wataalam kutoka nchi zote mbili kuanza kukutana kuanzia sasa kwa ajili ya kujadili mpango wa ujenzi wa bomba hilo na kumwalika Waziri wa Mafuta wa Kongo,  Mhe Aime Ngoi-Mukena Lusa- Diese kwenye kikao cha Mawaziri wa Nishati na Madini kutoka nchi za Tanzania na Uganda kinachotarajiwa kufanyika Tanga mapema mwezi Oktoba. 
Katika hatua nyingine Profesa Muhongo alisema kuwa nchi ya Kongo imeonesha nia kwenye utafiti wa mafuta katika Ziwa Tanganyika na kuongeza kuwa Serikali ipo tayari kushirikiana na nchi ya Kongo kupitia kampuni za utafiti na uchimbaji wa mafuta na gesi ili kuongeza kasi ya ugunduzi wa mafuta katika ziwa hilo lenye viashiria vya mafuta. 
Aidha alisisitiza kuwa mara baada ya ugunduzi wa mafuta katika Ziwa Tanganyika, nchi za Tanzania, Kongo na Burundi zitanufaika kupitia mapato pamoja na kuongezeka kwa ajira.
Waziri wa Mafuta wa Jamhuri ya Demokrasia ya  Kongo, Aime Ngoi-Mukena Lusa- Diese (kushoto) akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili kwenye Ofisi za Wizara ya Nishati na Madini. Kulia ni Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo.
Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo (kushoto) akiongoza kikao kilichoshirikisha Waziri wa Mafuta wa Jamhuri ya  Demokrasia ya  Kongo, Aime Ngoi-Mukena Lusa- Diese  na ujumbe wake, pamoja na  wataalam  kutoka Wizara ya Nishati na Madini.
Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akielezea fursa za uwekezaji kwenye sekta ya  mafuta na gesi mbele ya waandishi wa habari. Kushoto ni Waziri wa Mafuta wa Jamhuri ya Demokrasia ya  Kongo, Aime Ngoi-Mukena Lusa- Diese.
Mkurugenzi kutoka Kampuni ya Oil of DR Kongo kutoka Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, Giuseppe Ciccarelli akisisitiza jambo katika kikao hicho.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akipeana mikono  na Waziri wa Mafuta wa Jamhuri ya Demokrasia ya  Kongo, Aime Ngoi-Mukena Lusa- Diese (kushoto)

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...