SHIRIKISHO
la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limefungua kozi ya ukocha wa
magolikipa ambapo Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) limeipa
nafasi Tanzania kuwapa mafunzo ya juu ya ukocha wa makipa (Advanced
Goalkeeping Coach Course) ikiandika historia kuwa nchi ya pili barani
Afrika kwa makocha wa nafasi hiyo baada ya Botswana.
Makocha
wa makipa wapatao 25 kutoka timu za taifa, timu zinazoshiriki Ligi
Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, wanahudhuria kozi hiyo inayoongozwa na
Alejandro Heredia ambaye ni Mkufunzi kutoka FIFA. Makocha hao ni Peter
Manyika (Taifa Stars ya Tanzania), Saleh Ahmed (Zanzibar Heroes);
Muharami Mohammed (Timu ya Taifa ya Vijana wenye umri wa chini ya miaka
17 - Serengeti Boys); Mohammed Silima (Timu ya Taifa ya Vijana Zanzibar)
na Elyutery Mhoery (Timu ya Taifa ya Wanawake - Twiga Stars) na
msaidizi wake ambaye pia anachezea JKT Queens, Fatuma Omary.
Wengine
ni makocha maarufu wa makipa wakiwamo Juma Pondamali (Young Africans);
John Bosco (Majimaji ya Songea); Salimu Tupa (Tanga); Bakari Ali Hamadi
(Wete Pemba – Zanzibar); Hafidh Muhidin Mcha (Mkoani Pemba – Zanzibar);
Mussa Wanena (Kagera Sugar); Juma Bomba (African Lyon), Adam Abdallah
Moshi (Simba SC), Idd Mwinchumu (Azam FC) na Hussein Tade (Seeb
Club-Oman/Toto African). Pia wamo Khalid Adams (Mwadui FC); Josia Steven
(Mbeya City); Herry Boymanda (Tanzania Prisons); Emmanuel Mwansile
(Polisi Morogoro); Ben Kalama (Stand United); Abdallah Said (JKT Ruvu);
Patrick Mwangata (Mtibwa Sugar); Augustin Malindi (Mkoa wa Kigoma);
Raphael Mpangala (Ndanda FC); Salimu Tupa (Tanga) na nAbdul Mgude
(Coastal Union ya Tanga).
Heredia
aliweza kutoa nasaha kwa makocha hao wakati akiwanoa na kusema kuwa
“Kinachohitajika sasa ni juhudi tu. Kozi hii haijafanyika pengine hapa
barani Afrika zaidi ya Botswana. Mjue kuwa mna bahati na mbinu hizi
mzitumie kuweza kujenga magolikipa wziri wataoleta tija baadae.”
Akitoa
nasaha wakati wa ufunguzi wa kozi hiyo, Makamu Rais wa TFF, Wallace
Karia aliishukuru FIFA na CAF kwa namna inavyoshirikiana na TFF katika
kuwapa kozio nyingi za makocha wa timu kwa wachezaji wa mbele, makocha
wa makipa na waamuzi wa madaraja tofauti. “Hakuna kipindi TFF imepata
kozi za makocha nyingi za makocha kama kipindi hiki cha uongozi wa Jamal
Malinzi,” anasema Karia na kuongeza: “Tumetoka kwenye kozi ya makocha
wa Daraja A sasa tuko kwenu. Lengo ni Tanzania kuwe na makipa wazuri.
Ninyi mtaleta makipa wazuri. Na hii ni kwa manufaa ya sasa na baadaye
kwa upende wetu, timu zetu na taifa kwa ujumla.”
Karia
aliwatia hamasa makocha hao wanaoshiriki kozi hiyo kuwa, mara baada ya
kozi hiyo ipo siku watakwenda kuwa wakufunzi nje ya mipaka ya nchi
kadhalika makocha ambao wanaweza kupata kazi mahala popote duniani hasa
ukizingatia walimu wa daraja lao wako Tanzania na Botswana tu.
Kadhalika,
Makamu huyo wa Rais wa TFF alielezea kuwa mpira wa miguu una changamoto
nyingi na nyingine husababishwa na watalaamu hao kubweteka kwa
mafanikio. “Hili ni tatizo. Tubadilike kifikra na kivitendo. Msilaze
damu, kuweni active (mahiri).”
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...