Na Greyson Mwase, Shinyanga

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani ameitaka kampuni ya Pangea Minerals Ltd ya Canada inayofanya shughuli za utafutaji wa madini ya dhahabu katika kijiji cha Mwakitolyo Mkoani Shinyanga kuachia sehemu ya Leseni yake ili eneo hilo litengwe na kumilikishwa Wachimbaji Wadogo.

Akizungumza na uongozi wa Mkoa wa Shinyanga pamoja na Wawakilishi wa Wachimbaji Wadogo pamoja na Uongozi wa Kampuni ya Pangea Minerals Ltd mkoani Shinyanga, aliitaka kampuni hiyo ambayo imeanza mazungumzo ya kuuza eneo hilo kwa kampuni ya Busolwa Mining Ltd, kuachia sehemu ya leseni yake yenye namba PL 5044/2008 ambayo kwa sasa wananchi wanaokadiriwa kufikia 3000 wanajishughulisha na uchimbaji mdogo wa dhahabu katika eneo hilo tangu mwaka 2011.

Alifafanua kuwa ili kuepuka mgogoro huo ambao umedumu kwa muda mrefu kati ya kampuni hiyo na wananchi hao, ni vyema kampuni hiyo itoe ushirikiano kwa kijiji hicho kwa kuachia sehemu ya leseni yake ili wananchi nao wapate maeneo ya kufanyia shughuli za uchimbaji wa madini.

Dk. Kalemani aliitaka kampuni hiyo kuachia eneo hilo kwa Kamishna wa Madini ifikapo Agosti 17, 2016 ambapo eneo hilo litaanza kugawanywa kwa wananchi kuanzia Septemba 2, 2016.

Wakati huohuo Naibu Waziri Kalemani aliwataka wachimbaji wadogo kuheshimu sheria za nchi na kukubali kuhamia eneo litakalotengwa kwa ajili yao ifikapo tarehe 2 Septemba, 2016.

Naye Mwakilishi na Mkurugenzi kutoka kampuni ya Pangea Minerals Limited Ltd, Deo Mwanyika alikubali maamuzi hayo na kueleza kuwa kampuni ipo tayari kukabidhi sehemu ya leseni hiyo ili iweze kutumiwa na wananchi.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga aliipongeza serikali kwa mikakati yake ya kusaidia wachimbaji wadogo kwa kuwapatia maeneo ya kujiajiri kwa ajili ya kujiongezea kipato.

Aliwataka Wachimbaji Wadogo kutojihusisha na vitendo vya kiharakati na kuwarubuni baadhi ya wachimbaji na kupinga juhudi za Serikali kwa kuchochea vurugu migodini badala yake wayatumie maeneo hayo waliyotengewa kwa shughuli za kiuchumi.

Eneo la Mwakitolyo ni kati ya maeneo yenge utajiri wa dhahabu hapa nchini yanayomilikiwa na kampuni ya Acacia kupitia kampuni yake tanzu ya Pangea Minerals Ltd.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini Dk. Medard Kalemani akisisitiza jambo katika moja ya vikao vyake.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...