Timu za wasichana zinazoshiriki mashindano ya Airtel Rising Stars mkoani Lindi tayakwa ukaguzi wakati wa ufunguziwa michuano hiyo iliyofanyika Nachingwea mwishoni mwa wiki.

 Katibu tawala wa wilaya ya Nachingwea Husna Sekiboko akiwaongoza viongozi wa soka mkoani Lindi kukagua timu za wasichana zinazoshiriki michuano ya Airtel Rising Stars mkoani humo.


 MKUU wa mkoa wa Lindi Mheshimiwa Godfrey Zambi amewapongeza wasichana mkoani humo kwa kujitokeza kwa wingi kushirikia mashindano ya soka kwa vijana chini ya umri wa miaka 17 ya Airtel Rising Stars.

Timu sita za wasichana zimejitokeza kushirikia michuano hiyo ya kubaini vipaji vya wanasoka chipukizi yaliyoanza kutimua vumbi katika mkoa huo mwishoni mwa wiki. Mkoa wa Lindi ni miongoni mwa mikoa inayoshirisha timu za wasichana pekee. 

Katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala wa wilaya ya Nachingwea Husna Sekiboko, Mheshimiwa Zambi amewataka wasichana kutambua kwamba katika dunia ya leo mpira wa miguu fursa ambayo watu wengi, pamoja na wanawake, wanaitumia kuboresha maisha yao.

“Mpira ni burudani, mpira hudumisha amani, umoja, urafiki na udugu lakini muhimu zaidi mpira wa miguu ni chanzo cha ajira kwa mamilioni ya vijana duniani”, alisema na kuwahimiza vijana hao kucheza kwa bidii ili kuendeleza vipaji vyao.

Aliwataka viongozi wa soka mkoa wa Lindi kuchagua wachezaji wenye vipaji ili kuuwezesha mkoa huo kufanya vizuri katika fainali za Taifa za Airtel Rising Stars zinatarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Septemba 6 hadi 11.

Alisema michuano ya Airtel Rising Stars inasaidia kubaini wachezaji wenye vipaji kutoka sehemu mbalimbali ambao bila mashindano haya wangeweza kupotea hivi hivi. Aliwataka viongozi wa soka mkoa humo kushirikiana na shirikisho la soka nchini (TFF) kuwalea na kuwaendeleza vijana wanaopatikana kupitia Airtel Rising Stars.

Akiongea katika hafla hiyo ya ufunguzi, Katibu wa chama cha Soka mkoani Lindi Ally Mkadeba alisema kuwa Airtel Rising Stars imetoa hamasa kwa wasichana wengi mkoani Lindi kucheza soka na kuonyesha vipaji vyao.

Kwa upande wake, Ofisa Uhusiano wa Airtel Tanzania Jane Matinde alisema kuwa kampuni yake inajivunia kuweza kutoa mchango katika soka la Tanzania. “Airtel Rising Stars imekuwa chanzo cha kutumainiwa kwa klabu na timu za Taifa kupata vijana chipukizi wenye vipaji. Tunaona fahari kuweza kupata fursa ya kudhamini soka nchini Tanzania“alisema Matinde.

Hafla hiyo ya ufunguzi ilishuhudia mchezo wa ufunguzi kati ya FT Vito Malaika na Nachingwea Academy ambapo FT Vito Malaika waliwaduwaza wapinzani wao kwa kuwatandika 4-0. Michuano ya Airtel Rising Stars ngazi ya mkoa pia inaendelea kutimua vumbi Zanzibar, Kinondoni, Temeke, Mwanza, Mbeya, Arusha na itafunguliwa Morogoro Jumatano.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...