Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Christina Mndeme (kushoto) akimshukuru mtoto Aisha Mshantu kwa Msaada wa madawati 50 yenye thamani ya shilingi milioni 5.2 aliyoyatoa katika shule ya Msingi Mwenge iliyopo Kata ya Mbabala Manispaa ya Dodoma.
Mtoto Aisha Mshantu (kulia )akimkabidhi madawati 50 yenye thamani ya shilingi milioni 5.2 Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Christina Mndeme aliyoyatoa katika shule ya Msingi Mwenge iliyopo Kata ya Mbabala Manispaa ya Dodoma.
Mtoto Aisha Mshantu na wazazi wake Mzee Mshantu (wa kwanza kulia) na Bi Rehema (wa pili kulia) wakiwa amekaa katika madawati aliyoyatoa mtoto huyo kama msaada katika shule ya Msingi Mwenge iliyopo Kata ya Mbabala Manispaa ya Dodoma. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Christina Mndeme.
NA RAMADHANI JUMA,
DODOMA
KATIKA hali isiyotegemewa msichana mdogo Aisha Mshantu ambaye ni muhitimu wa kidato
cha sita mwaka 2016 ameitikia wito wa Mheshimiwa Rais Dokta John Magufuli wa kuwaomba
wadau kushiriki katika zoezi la kuchangia madawati kwa ajili ya wanafunzi wa shule za Msingi
na Sekondari nchini ili waondokane na adha ya kujifunza wakiwa wameketi chini.
Aisha ametoa madawati 50 yenye thamani ya shilingi milioni 5.2 katika shule ya Msingi ya
Mwenge iliyopo katika kijiji cha Mbabala A Kata ya Mbabala Manispaa ya Dodoma, ambapo
amesema hiyo ni ndoto yake ya muda mrefu na kwamba anafuraha kuikamilisha ili kuonesha
alivyoguswa na tatizo la wanafunzi kukaa chini wakati wa kujifunza.
Mbali na msaada huo wa madawati, msichana huyo ambaye amezaliwa akiwa mlemavu, pia
ametoa msaada wa mataulo maalum 84 kwa ajili ya wanafunzi wa kike katika shule hiyo yenye
thamani ya shilingi laki mbili, kama chachu ya kuwazindua wasijiingize katika masuala ya
mahusiano kwa kudanganywa na wanaume kwa kuahidiwa mahitaji madogo.
Akizungumza katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika shuleni hapo juzi baada ya kupokea
misaada hiyo kwa niaba ya Serikali na Manispaa ya Dodoma, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma
Christina Mndeme alimshukuru mtoto Aisha kwa msaada huo ambapo alisema msichana huyo
ameonesha uzalendo wa hali ya juu kwa watoto wenzake huku akitoa wito kwa jamii kujifunza
kutokana na tukio hilo.
“Hakuna fedha isiyokuwa na kazi..Aisha ana mahitaji yake na angeweza kuzitumia fedha hizi
kwa matumizi mengine ya binafsi lakini yeye ameamua kusaidia wadogo zake wa shule ya
Msingi..hili ni jambo la kijasiri sana kwa mschana mdogo kama huyu na ni funzo kubwa kwa
jamii nzima” alisema.
Akielezea ndoto aliyokuwa nayo mtoto wake kwa muda mrefu, mama mzazi wa Aisha Bi
Rehema alisema mtoto wake huyo alifungua akaunti ya ‘Jumbo Junior’ katika Benki ya CRDB
Dodoma na kuanza kujiwekea akiba kidogo kidogo hadi alipofikia azima yake hiyo.
Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma Felister Bura ameahidi kukarabati darasa moja
katika shule hiyo ambako madawati hayo yatatumika, ikiwa ni hatua ya kuunga mkono juhudi za
Msichana Aisha ambaye kwa sasa ni Balozi wa Elimu wa Umoja wa Mataifa (UN) kupitia
programu ya ‘4 Quality Education’.
Kazi nzuri Aisha ya kuchangia maendeleo ya elimu nchini kwako.
ReplyDeleteMasha Allah! Mwenyeez Mungu akuzidishie maradufu 'Saba Wa Sabiini' Mtoto Mzuri Bi Aisha Mshantu kwacho ulichojaaliwa kuchangia, kwani si haba utakuwa umekidhi haja husika. Kwa kweli hongera sana na pongezi za dhati kwa kujitolea ikiwa ni mfano mzuri kwani pia umeweza kuonyesha kuwa unajali suala zima la elimu na umuhimu wake, khususan kwa watoto wenzako, kadhalika katika kuuitikia wito huo wa uchangiaji wa madawati nchini. Mwenyeez Mungu akuzidishie moyo huo huo wa imani, upendo na kujitolea. Naamini hilo litahamasisha na watoto wengine ambao kwa niaba ya wazazi wenye uwezo wa kuwawezesha, basi nao wakaweza kuiga mfano huo. Mungu Ibariki Tanzania.
ReplyDelete