Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 16 Agosti, 2016
amewatembelea na kuwajulia hali Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Mhe. Job Ndugai na Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. John Samuel Malecela Jijini Dar es Salaam.
Pamoja na
kuwajulia hali, Rais Magufuli aliyeongozana na Mkewe Mama Janeth Magufuli
amewaombea kwa Mwenyezi Mungu wapone na kupata nguvu haraka ili waweze
kuendelea na majukumu yao ya kawaida katika ujenzi wa Taifa.Akizungumza na
Rais Magufuli nyumbani kwake Salasala Jijini Dar es Salaam spika wa Bunge Mhe.
Job Ndugai amemshukuru Rais Magufuli kwa kumtembelea, kumjulia hali na
kufuatilia kwa ukaribu wakati wote alipokuwa akipata matibabu nchini India hadi
aliporejea hapa nchini.
"Kwa kweli
nimefarijika sana, kwanza naomba nimshukuru sana Mhe. Rais kwa sababu
nilipopata matatizo haya ya maradhi alikuwa karibu sana na mimi nikiwa hapa
nchini na hata nilipopelekwa nchini India alinipigia simu mara kwa mara na
kunifariji sana, na hapa amekuja kuniona kwa niaba ya watanzania kwa kweli
namshukuru sana na namuombea kwa Mwenyezi Mungu aendelee kumpa moyo huu wa
kuwajulia hali wale wenye matatizo mbalimbali"Lakini
niwahakikishie Watanzania, kwamba kwa sasa nina nafuu kubwa sana, naweza
kufanya kazi nyingi tu sasa lakini tuendelee kuombeana" Ameeleza
Mhe. Ndugai alipokuwa akizungumzia hali yake kwa sasa.
Kwa upande wake Makamu
wa Rais Mstaafu na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. John Samuel Malecela pamoja na
kumshukuru Rais Magufuli na Mkewe Mama Janeth Magufuli kwa kumtembelea amesema
afya yake inazidi kuimarika na pia amewashukuru Madaktari wanaompatia matibabu.
"Mheshimiwa
Rais nakushukuru sana, namshukuru pia Mama Janeth Magufuli kwa kunitembelea na
kunifariji, naendelea vizuri na matibabu na afya yangu imeimarika kwa kiasi
kikubwa" Ameeleza Mhe. Malecela.
Gerson
Msigwa
Kaimu Mkurugenzi
wa Mawasiliano, IKULU
Dar es
Salaam
16 Agosti,
2016.
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana kwa
furaha na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai mara baada
ya kuwasili nyumbani kwake Sala sala nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Mke wake
Mama Janeth Magufuli kushoto akizungumza jambo na Spika wa Bunge la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Job Ndugai nyumbani kwake Sala sala jijini Dar es Salaam
walipokwenda kumjulia hali. Kulia ni mke wa Spika Dkt. Fatma Mganga Ndugai.
Mke
wa Rais Mama Janeth Magufuli akisalimiana na
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai mara baada
ya kuwasili nyumbani kwa Spika Sala sala jijini Dar es Salaam.
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimjulia hali
Waziri Mkuu mstaafu John Samuel Malecela ambaye anapata matibabu jijini Dar es
Salaam.
Mke
wa Rais Mama Janeth Magufuli akiwa pamoja na Rais Dkt. John Pombe Magufuli
akiongoza Sala ya kumuombea Waziri Mkuu mstaafu John Samwel Malecela pamoja na
mkewe Anne Kilango Malecela.
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiagana na mke wa
Spika Dkt. Fatma Mganga Ndugai huku Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akiagana
na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai mara baada ya
kuwajulia hali nyumbani kwao Sala sala jijini Dar es Salaam. PICHA NA IKULU
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...