Serikali imesema itaunga mkono juhudi zinazofanywa na Benki ya Letshego zinazolenga kupunguza umaskini na kuongeza ustawi wa kifedha kwa Watanzania kwa kutoa huduma za kifedha kwa watu walio na kipato cha chini na wasiyofikiwa na huduma hizo maeneo ya vijijini.

Hayo yalisemwa na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba ambaye alikuwa mgeni rasmi wakati wa sherehe ya kutimiza miaka 18 ya utoaji huduma barani Afrika na kutimiza miaka 10 hapa Tanzania ikitoa huduma kwa jina la FAIDIKA, sherehe iliyoambatana na chakula cha jioni iliyofanyika jijini Dar es Salaam juzi jioni.

Waziri Mwigulu alisisitiza kwamba mikakati ya Serikali ya awamu ya tano inalega katika kujumuisha kila mmoja na kila Mtanzania kushiriki katika ajenda ya maendeleo.

"Nimefurahi kuona Letshego ikijidhatiti kutoa huduma pana za kifedha na kusaidia wateja walioko vijijini na wale wasiofikiwa na huduma za kibenki waishio mikoani na nnje ya miji mikuu ya hapa nchini Tanzania. Natoa wito kwa mashirika mengine kufuata mifano ya Letshego," alisema Mwigulu ambaye aliwahi kushika nafasi ya Naibu Waziri wa Fedha.

Alisema Serikali inafaraja kuona jinsi Letshego pia inashiriki katika kuja na ufumbuzi wa huduma za kifedha ambazo zinalenga kuchochea ukuwaji wa sekta mbali mbali ikiwa ni pamoja na kilimo, afya, maendeleo ya makazi, elimu, biashara ndogo ndogo na za kati na uwekezaji kwenye jamii.

Aidha, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Letshego Holdings Limited Group Bw. Chris Low, alisema taasisi hiyo (ambayo Letshego Bank (T) Limited ni kampuni tanzu yake) inalenga kuwa kinara katika utoaji wa huduma jumuishi wa kifedha kwa makundi yote barani Afrika.

"Tumetengeneza msingi imara ya biashara ambayo itatuwezesha kufikia dhamira yetu. Mafanikio yatakuja kupitia watu wetu na kwa kufanya kazi kama timu, itahitaji kuendelea kukua, kuangalia utofauti wetu kwa mtazamo chanya, pamoja na kutekeleza ahadi yetu ya kuboresha maisha", alisema Bw Chris.

Alisema Letshego imekuwepo hapa nchini Tanzania ikijulikana kama FAIDIKA kwa takriban miaka 10, ambapo wamekuwepo na wawakilishwa katika mikoa yote na matawi 110 zilizosambaa katika angalau asilimia 95 ya wilaya zote.

"Katika mwaka wa 2015, kwa msaada na idhini ya Benki Kuu ya Tanzania tulifanikisha ununuzi wa hisa asilimia 75 katika benki ya Advans ya Tanzania, benki ya kibiashara yenye matawi matano (5), ambayo ililenga katika utoaji wa huduma za kubenki kwa wajasiriamali wadogo na wakati.

"Kwa biashara zetu zilizopo, Faidika na sasa benki ya Letshego, tukotayari kuwatumikia wateja zaidi ya 70,000 na tuna matarajio ya kuchukua jukumu la kuendeleza ajenda ya ushirikishwaji wa pamoja katika huduma za kifedha ambayo Serikali ya Tanzania inakuza," alisema Mkurugenzi wa taasisi hiyo.

Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba (wa pili kulia) akizindua muonekano mpya wa Benki ya Letshego (iliyojulikana awali kama Advans Bank) wakati wa hafla ya usiku iliyofanyika Jumatano jijini Dar es Salaam. Wa kwanza kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Letshego Holdings Limited Group Bw. Chris Low. Kushoto ni Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Letshego Holding Bw. Hannington Karuhanga na wa pili kushoto ni Afisa Mkuu wa Benki ya Letshego ya Tanzania Bw. Yohane Kaduma. 
Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba (wa pili kulia) akimpongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Letshego Holdings Limited Group Bw. Chris Low (wa kwanza kulia) baada ya kuzindua muonekano mpya wa Benki ya Letshego (iliyojulikana awali kama Advans Bank) wakati wa hafla ya usiku iliyofanyika Jumatano jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Letshego Holding Bw. Hannington Karuhanga na wa pili kushoto ni Afisa Mkuu wa Benki ya Letshego ya Tanzania Bw. Yohane Kaduma.
Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba (wa pili kulia) akimpongeza Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Letshego Holding Bw. Hannington Karuhanga (kuashoto) baada ya kuzindua muonekano mpya wa Benki ya Letshego (iliyojulikana awali kama Advans Bank) wakati wa hafla ya usiku iliyofanyika Jumatano jijini Dar es Salaam. Wa kwanza kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Letshego Holdings Limited Group Bw. Chris Low na wa pili kushoto ni Afisa Mkuu wa Benki ya Letshego ya Tanzania Bw. Yohane Kaduma.

Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba (mwenye tai yenye rangi za bendera ya Taifa) akifurahia jambo pamoja na wageni na washiriki katika uzinduzi wa muonekano mpya wa Benki ya Letshego (iliyojulikana awali kama Advans Bank) wakati wa hafla ya usiku iliyofanyika Jumatano jijini Dar es Salaam.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. Jina la benki 'mtaliki mwanamke huyo'

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...