Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amesema ujenzi wa reli ya kisasa (standard gauge) unatarajiwa kuanza mwezi Desemba mwaka huu na kama ilivyo miradi mikubwa unatarajiwa kukamilika ndani ya miaka mitatu na utajengwa kwa awamu nne ili kuharakisha kukamilika kwake.

Waziri Prof. Mbarawa amesema Prof. Mbarawa ametoa kauli hiyo leo, wakati wa Mkutano wa Sita uliowakutanisha  Mawaziri wa Sekta ya Uchukuzi wa nchi za Tanzania, Rwanda na Burundi, uliofanyika jijini Dar es Salaam ambapo amesema lengo la mkutano huo ni kuangalia namna bora ya kupunguza vikwazo kwenye sekta hiyo baina ya nchi hizo.

Amesema kuwa ushirikiano baina ya nchi za Afrika Mashariki katika ujenzi wa reli hiyo utachochea kasi ya usafirishaji wa mizigo na shughuli za kibiashara na hivyo kuinua uchumi wa nchi hizo.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (katikati), akizungumza na viongozi mbalimbali wa sekta ya uchukuzi (hawapo pichani), katika Mkutano wa Sita wa Kamati ya Mawaziri wa nchi za Tanzania, Rwanda na Burundi uliofanyika jijini Dar es salaam. Kulia ni Waziri wa Uchukuzi wa Burundi Eng. Jeon Ntunzwenidana na kushoto ni Katibu Mkuu wa Sekta ya Uchukuzi ya Tanzania Dkt. Leonard Chamuriho.

“Kama mnavyojua Serikali imetenga kiasi cha shilingi Trilioni moja kwa ajili ya kuanza kutekeleza mradi huo na wenzetu nao watatafuta fedha katika nchi zao ili kukamilisha ujenzi wake”, amesema Waziri Prof. Mbarawa.

Aidha Prof. Mbarawa amebainisha kuwa kila nchi itatekeleza mradi wa kujenga reli ya kisasa kwa sehemu yake hivyo ni wajibu wa kila nchi kukamilisha mradi huo ili kuchochea maendeleo yanayotokana na Sekta ya Uchukuzi.

Amesema kwa upande wa nchi ya Tanzania reli hiyo itaanza kujengwa kuanzia Dar es Salaam- Tabora-Isaka hadi Mwanza yenye urefu wa KM 1,219 ambayo ndiyo uti wa mgongo wa reli yenyewe. Sehemu nyingine ni kutoka Tabora-Mpanda- Kalemela; Tabora-Uvinza hadi Kigoma. Katika kuunganishwa na nchi ya Rwanda na Burundi, Waziri Mbarawa amesema ujenzi wa reli hiyo itajengwa kuanzia Isaka-Rusumo mpaka Kigali na Keza mpaka Musongati.
Katibu Mkuu wa Sekta ya Uchukuzi Dkt. Leonard Chamuriho akifafanua jambo kwa viongozi mbalimbali wa sekta ya uchukuzi (hawapo pichani), katika Mkutano wa Sita wa Kamati ya Mawaziri wa nchi za Tanzania, Rwanda na Burundi uliofanyika jijini Dar es salaam. Kulia ni Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa.

Naye Waziri wa Uchukuzi wa nchi ya Burundi Eng. Jeon Ntunzwenidana amefurahishwa na Serikali ya Tanzania katika jitihada zake za kuharakisha ujenzi wa reli hiyo na amesema Serikali ya Burundi itakamilisha ujenzi huo haraka ili kurahisisha usafirishaji wa mazao na huduma za kibiashara baina ya nchi hizo.

Waziri Prof. Mbarawa amesaini makubaliano ya uboreshwaji wa sekta ya mawasiliano, reli na barabara baina ya nchi za Tanzania, Rwanda, Burundi, Uganda na Jamhuri ya Demokrasia ya Congo (DRC).

Zaidi ya trilioni 16 zinatarajiwa kutumika katika ujenzi wa reli ya kisasa nchini Tanzania yenye takribani urefu wa KM 2,600.
Viongozi wa Sekta ya Uchukuzi wakijadiliana kuhusu changamoto mbalimbali za sekta hiyo katika Mkutano wa Sita wa Kamati ya Mawaziri wa nchi za Tanzania, Rwanda na Burundi uliofanyika jijini Dar es salaam.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya Mkutano wa Sita wa Kamati ya Mawaziri wa nchi za Tanzania, Rwanda na Burundi uliofanyika jijini Dar es salaam.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa pili kulia) pamoja na mawaziri kutoka nchi shiriki wakisaini makubaliano ya uboreshwaji wa sekta ya mawasiliano, reli na barabara baina ya nchi za Tanzania, Rwanda, Burundi, Uganda na Jamhuri ya Demokrasia ya Congo (DRC).

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...