Na Eleuteri Mangi-MAELEZO, Dodoma

Serikali imewasilisha Miswada miwili inayohusu Sheria ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali wa mwaka 2016 na ule wa Sheria ya Usimamizi wa Wanataaluma wa Kemia wa mwaka 2016 ambayo imesomwa kwa mara ya pili Bungeni ili ijadiliwe na wabunge.

Awali akisoma Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali wa mwaka 2016, Wizari wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalim amesema kuwa madhumuni ya Muswada huo ni kuanzisha Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na kuweka kisheria majukumu yake.

Aidha, Waziri Ummy amesema kuwa Muswada huo umezingatia masuala mbalimbali ikiwemo kuanzishwa kwa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali pamoja na kuainisha majukumu yake na kuanzisha Bodi ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali.

Mambo mengine yaliyozingatiwa katika Muswada huo ni kubainisha utaratibu wa uteuzi wa Mkemia Mkuu wa Serikali, majukumu yake na mamlaka yake, kuifanya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kuwa maabara ya rufaa na msemaji wa mwisho wa Serikali katika shughuli za uchunguzi wa kimaabara wa kikemia, sayansi jinai na vinasaba na Muswada huo utawwzesha kuwekwa utaratibu wa kusajili, kuratibu na kusimamia maabara na shughuli zote za maabara za kikemia, sayansi jinai na vinasaba.

Zaidi ya hayo, Waziri Ummy amesema kuwa kupitia Muswada huo kitawekwa kifungu maalum chini ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kitakachogharimiwa na Serikali kwa ajili ya uchunguzi wa vielelezo vya makosa ya jinai, majanga na masuala mengine yenye maslahi ya taifa ili kuwezesha utekelezaji wa jukumu hilo kwa ufanisi hali itakayosaidia utoaji wa haki katika vyombo vya maamuzi na kuleta utengamano katika jamii.

Aidha, Muswada wa pili uliowasilishwa unahusu Sheria ya Usimamizi wa Wanataaluma wa Kemia wa mwaka 2016 ambapo maoni na ushauri yaliyotolewa na Kamati ya kudumu ya Bunge ya Huduma ya Maendeleo ya Jamii yaliyosawilishwa na Jasmin Tisekwa (Mb) kwa niaba ya Mwenyekiti wakamati hiyo Peter Serukamba amesema kuwa Muswada huo utasaidia kutungwa kwa sheria ambayo italeta tija kwa maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Zaidi ya hayo, Jasmini amesema kuwa Muswada huo utasaidia wanataaluma ya Kemia kukabiliana na maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja kwa kuzingatia taaluma hiyo kwani ina mchango mkubwa katika maendeleo ya sekta za elimu, kilimo, viwanda, sheria, afya, mazingira na jamii kwa ujumla wake. 

Akisoma maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Waziri Kivuli wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ester Mtiko amepongeza jitihada zinazofanywa na wataalamu wa kemia katika sekta mbalimbali kwa kuwa wana wajibu mkubwa kwa maslahi ya taifa kwa ajili ya usalama na kuendeleza maarifa ya kisayansi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...