Kamishna wa Polisi Kanda Maalum Dar Es Salaam anatoa rai kwa wakazi wa
Jiji la Dar Es salaam na wageni wanaoingia jijini wakitokea mikoani
kupuuza taarifa za sauti zinazozagaa katika mitandao ya kijamii kuwa
Polisi wanawakamata ovyo watu wanaolala kwenye nyumba za kulala wageni.
Taarifa
hizo za uvumi zinazoendelea kuzagaa kwenye mitandao ya Kijamii kama
WHATSAPP, TELEGRAM na pia zimechapishwa kwenye baadhi ya magazeti kwamba
Askari Polisi wanawakamata watu ovyo mchana wakiwa kwenye nyumba za
kulala wageni kwa madai ya kukamata kwa makosa ya uzembe na uzururaji
na pia kutimiza kauli ya Raisi wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania ‘HAPA
NI KAZI TU’.
Kimsingi niwatoe hofu raia wema kuwa tunaendelea na
oparesheni za kuwasaka watuhumiwa wa makosa mbalimbali yakiwemo
wanaofanya biashara ya nyumba za kulala wageni kinyume cha sheria (guest
bubu), majambazi na wahalifu wengine wa makosa mbalimbali.
Aidha
taarifa za kuaminika zimebaini kuwa baadhi ya nyumba za kulala wageni
zimekuwa zikitumika kuhifadhi magenge ya wahalifu, dada poa na kaka poa,
hivyo Jeshi la Polisi tunawajibika kufuatilia na kuwakamata wahalifu.
Niwajibu
wa Polisi kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwenye nyumba za kulala
wageni, Hoteli, migahawa, Vilabu vya vileo, kumbi za starehe
zinazokesha na zisizokesha na watakaobainika kuvunja sheria, hatua kali
za kisheria dhidi yao zitachukuliwa. Sheria ya Mwenendo ya makosa ya
jinai kifungu cha 60(1) (sura ya 77 iliyofanyiwa marekebisho 2002)
kinampa nguvu askari kufanya ukaguzi wa maeneo yote yaliyotajwa hapo juu
na kumkamata mtu yeyote anayetiliwa shaka akienda kinyume na utaratibu
wa biashara hizo.
Sambamba na hayo nawatahadharisha
wafanyabiashara wote wa nyumba za kulala wageni wafuate taratibu za
kupokea wageni kwa kuandika kwenye vitabu, kuandika namba za
vitambulisho vyao na sehemu wanayotoka, na pale watakapomtilia mashaka
mteja yeyote watoe taarifa kituo chochote cha polisi.
Pia
wenyeviti wa serikali za mitaa na wajumbe wa nyumba kumi wanawajibika
kuwatambua wageni wote wanaoingia kwenye himaya zao na kuwachukulia
hatua stahiki ili kuimarisha usalama katika jiji letu la Dar Es salaam.
DAR ES SALAAM BILA UHALIFU INAWEZEKANA, TUSHIRIKIANE KUISAFISHA JIJI LETU
S.N.SIRRO - CP
KAMISHNA WA POLISI
KANDA MAALUM
DAR ES SALAAM
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...