Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mh. January Makamba akiongea na waandishi wa Habari juu ya Siku ya Kimataifa ya tabaka la Ozoni. Siku hii huadhimishwa Septemba 16 kila mwaka. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mazingira Bw. Richard Muyungi. (Picha kwa hisani ya Idara ya Habari Maelezo)
…………………………………………………………..
Tarehe 16 Septemba mwaka huu tutaungana na Jumuiya ya Kimataifa kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Hifadhi ya Tabaka la Ozoni kama ilivyoagizwa na Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Azimio lake nambari 49/114 la tarehe 19 Desemba 1998 kama kumbukumbu ya tarehe ya kutiwa saini Mkataba wa Montreal (Montreal Protocol – 1987) kuhusu kemikali zinazomong’onyoa Tabaka la Hewa ya Ozoni angani.

Ozoni ni hewa iliyoko kwenye angahewa ya juu, takribani kilometa 10 hadi 50 juu ya ardhi. Kazi yake kubwa ni kuchuja sehemu kubwa ya mnururisho wa mionzi kama “Ultraviolet B” isifike kwenye uso wa dunia. Ujumbe wa mwaka huu ni “Kuhuisha Tabaka la Ozoni na Tabia-Nchi kwa pamoja Duniani”. Ujumbe huu umeambatana na Kauli mbiu isemayo “Kukabiliana na ongezeko la gesi Joto Duniani HFCs chini ya Itifaki ya Montreal”. 

Tabaka la Ozoni linapoharibiwa huchangia kuruhusu mionzi zaidi ya “Ultraviolet B” kufika kwenye uso wa dunia na hivyo kusababisha kuongezeka kwa magonjwa kama vile saratani ya ngozi, uharibifu wa macho yaani “mtoto wa jicho” unaosababisha upofu, upungufu wa kinga dhidi ya maradhi na kujikunja kwa ngozi. Aidha, madhara mengine ni kuharibika kwa mimea hasa mazao ya kilimo kutokana na kuathirika kwa maumbile na mifumo ya ukuaji. 
 
Vile vile, baadhi ya kemikali hizi husababisha kuongezeka kwa joto duniani na hivyo kuchangia katika mabadiliko ya tabianchi.
Ili kulinda tabaka la Ozoni, Serikali za mataifa mbalimbali zilikubaliana kuunda Mkataba wa Vienna (Vienna Convention) wa Hifadhi ya Tabaka la Ozoni mwaka 1985. Mkataba huu unasisitiza ushirikiano katika utafiti, usimamizi na ubadilishanaji wa taarifa za hali ya Tabaka la Ozoni kutokana na kupungua kwa matumizi yake. 
 
Vile vile ulianzishwa Mkataba wa Montreal (Montreal Protocol) unaohusu udhibiti wa kemikali zinazomong’onyoa Tabaka la Ozoni na Mkataba huu ulipitishwa tarehe 16 Septemba, 1987. Lengo kuu la Mkataba huu ni kuhifadhi Tabaka la Ozoni kwa kudhibiti utengenezaji na matumizi ya kemikali zinazoharibu Tabaka hili. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...