Tanzania imekubali kuyatekeleza mapendekezo 131, kuyakataa 94, kuyakubali kiasi mawili kati ya mapendekezo 227 yaliyotolewa na mataifa wanachama wa Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa. Taarifa ya Serikali iliwasilishwa mbele ya Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria Profesa  Sifuni Mchome (pichani) lililokaa September 21 hadi 23, 2016.
Aidha, Baraza hilo limepitisha Taarifa hiyo ya pili ya Tanzania ya Haki za Binadamu chini ya Mfumo wa Mapitio wa Umoja wa Mataifa kwa Kipindi Maalum (Universal Periodic Review (UPR) Mechanism) katika kikao kilichofanyika mjini Geneva nchini Uswisi.
Mapendekezo ambayo Tanzania imeyakubali yanahusu; ukamilishaji wa Mchakato wa Katiba, kuijengea uwezo wa kifedha Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, kutekeleza Malengo endelevu ya Dunia, Uandaaji wa Taarifa za Nchi za Utekelezaji wa Masuala ya Haki za Binadamu, Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Haki za Binadamu, haki za wanawake na watoto, watu wenye ulemavu, wazee, haki ya elimu, afya, maji, mazingira na mengineyo.
Aidha, Mapendekezo mawili  ambayo yalikubaliwa nusu yalikuwa na baadhi ya mambo ambayo yanaendana na Katiba, Sera na Sheria za nchi na mambo mengine ambayo yanakinzana na hayo. Masuala hayo yanahusu Serikali kuziwezesha Asasi za Kiraia kimuundo na kifedha na kutoa fidia kwa wahanga wanaotokana na mashambulizi yanayofanywa kwa watu wenye ualbino.
Mapendekezo ambayo Tanzania imeyakataa yanahusu suala la hali ya kisiasa Zanzibar, Sheria ya Makosa ya Mtandaoni, uhuru wa kupata taarifa , adhabu ya kifo, utoaji mimba, mapenzi na ndoa za jinsia moja, ubakaji ndani ya ndoa na umiliki wa ardhi kwa kuwa yanakwenda kinyume na Katiba, Sheria, Sera, Dini na Tamaduni za nchi kwa ujumla.
Akiwasilisha taarifa hiyo ya Serikali, Prof Mchome amesema Serikali imejidhatiti kutekeleza mapendekezo yote yaliyokubaliwa na kuongeza kuwa Tanzania inaunga mkono Azimio la Vienna na kwamba itaendelea kutekeleza mpango wa Taifa wa Haki za Binadamu.
“Tumejidhatiti kutekeleza mapendekezo tuliyoyakubali na tutaendelea kuimarisha taasisi ya Taifa ya Haki za Binadamu kwa kuipatia rasilimali fedha, watu na vifaa ili ifanye kazi ya kuwaletea wananchi maendeleo kwa mtindo wa haki za binadamu,” alisema.
Pia alisema kuwa kuna baadhi ya mapendekezo ambayo Serikali imeyachukua kwa ajili ya kuyafanyia kazi. Mapendekezo hayo ni pamoja na haki za watu wenye ualbino, adhabu ya viboko na haki ya mtoto kuandikishwa bure baada ya kuzaliwa ili apatiwe cheti cha kuzaliwa.
Profesa Mchome alisema Serikali imepokea mapendekezo matatu kuhusu haki za watu wenye ualbino ambayo yanataka Serikali kuifanyia mabadiliko Sheria ya Dawa na Tiba Mbadala ya mwaka 2002 ili kuwazuia waganga kutowadhuru watu wenye ualbino na kuahidi kuwa wataipitia upya.

Alisema kuwa Serikali imepokea na kukubali sehemu ya pendekezo la kuzisaidia kifedha na kimuundo asasi zinazojishughulisha na masuala ya watu wenye ualbino. “Tumepokea na kukubali sehemu ya pendekezo hilo ambalo linaitaka Serikali kuzisaidia kifedha na kimuundo asasi zinazojishughulisha na masuala ya watu wenye ualbino,” alisema.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...