Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe Mhandisi Methew Mtigumwe akimkabidhi Mwenge wa Uhuru Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey D.J Mwanri (Kulia)
Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe Mhandisi Methew Mtigumwe akisoma Risala wakati wa makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru.
Na Mathias Canal, Tabora.

MWENGE wa Uhuru umewasili Mkoani Tabora ambapo unatarajiwa kuzindua miradi 45 yenye thamani ya shilingi Bilioni ishirini na tatu, Milioni nne, laki nne elfu na arobaini na saba mia tano sitini na sita 23,004,447,566/= ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 40% ukulinganisha na miradi ya mwaka 2015 iliyokuwa na thamani ya shilingi 9,207,720,213.

Akizungumza wakati wa makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru katika Kijiji cha Mgongolo, Kata ya Igunga, Wilayani Igunga Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey D.J Mwanri amesema kuwa sera ya Vijana Tanzania ya Mwaka 2007 inatambua kuwa vijana ni watu wote wenye umri wa miaka 15-35 ambapo kulingana na sensa ya Mwaka 2012 inaonyesha kuwa Mkoa huo una jumla ya vijana 439,455 hivyo hekari 681 zimetengwa kwa ajili ya shughuli za vijana ili kukidhi kauli mbiu ya Mwenge wa Uhuru mwaka 2016.

Mwanri alisema kuwa Mwaka 2015 Mwenge wa Uhuru mkoani Tabora ulikimbizwa katika Halmashauri 7 zilizokuwepo ambapo Mwaka huu utakimbizwa katika Halmashauri 8 ambazo ni Igunga, Nzega Mji, Tabora Vijijini (Uyui), Sikonge, Urambo, Kaliua, Tabora Manispaa na Nzega Vijijini.

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe Aggrey Mwanri mara baada ya kukabidhiwa Mwenge huo naye amemkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Igunga Mhe John Mwaipopo ili aukimbize katika Miradi iliyopangwa ukiwemo wa kuzindua Mradi wa maji Vijijini, Kufungua vyumba viwili vya madarasa na choo cha matundu 10 katika Shule ya Sekondari Mwayunge, Kuweka Jiwe la msingi katika Hoteli ya Mjasiriamali Zengo T. Kija, Kuzindua mradi wa Kilimo cha bustani na Ufugaji wa samaki wa kikundi cha Vijana cha Msongela, na Kuzindua zahanati ya Kijiji cha Igogo.

Miradi mingine ambayo Mwenge wa Uhuru utazuru ni pamoja na kugawa kadi za CHF kwa wanachama wapya, Kugawa vyandarua kwa wananchi na baadaye utazuru katika Shule ya Sekondari Nanga.

Akizungumza wakati wa kukabidhi Mwenge wa Uhuru kwa uongozi wa Mkoa wa Tabora, Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe Mhandisi Mathew J. Mtigumwe amewashukuru wananchi wa Mkoa wa Singida kwa kujitokeza kwa wingi kutokana na juhudi na ushiriki wao kwenye kuibua, Kutekeleza na Kusimamia miradi mbalimbali ambapo pia amewataka wananchi hao kwa umoja wao kuitunza miradi hiyo.

Mtigumwe alisema kuwa tangu Mwenge wa Uhuru ulipokabidhiwa Mkoani Singida ukitokea Mkoani Dodoma Septemba 17, 2016 umepita kwenye miradi 61yenye thamani ya Shilingi 14,266,628,518 iliyopo katika Halmashauri saba ambayo ni pamoja na Mradi wa elimu, Afya, Maji, Barabara, Biashara, Mazingira, Kilimo, Mifugo, Ushirika na programu mbalimbali za mapambano dhidi ya Rushwa, Dawa za Kulevya, Ukimwi na Malaria.

Mtigumwe alisema kuwa mbali na Mwenge wa Uhuru kupita kwenye Miradi mbalimbali Mkoani Singida Kiongozi wa mbio za Mwenge Kitaifa amewaongoza wakimbiza Mwenge wenzake kitoa ujumbe wa Mwenge wa Uhuru wa mwaka 2016 ambao ni "Vijana ni nguvu kazi ya Taifa, Washirikishwe na kuwezeshwa" Vile vile, Kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa amesisitiza umuhimu wa vijana na wananchi wote kwa ujumla kujiepusha na vitendo vya Rushwa, Dawa za kulevya, Kuchukua hatua dhidi ya tabia hatarishi zinazoweza kuchochea maambukizi mapya ya Virusi vya Ukimwi na kutokomeza kabisa ugonjwa wa Malaria.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...