Na Immaculate Makilika
 na Abushehe Nondo - MAELEZO
WAKUU wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wamekubaliana kutumia kipindi cha miezi 3 hadi Januari mwakani ili kuupitia upya mkataba wa mahusiano ya kiuchumi na kibiashara kati ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki na Ulaya (EPA) kabla ya kukubaliana na baadhi ya vipengele vya mkataba huo. 
 Akizungumza katika mkutano wa dharura wa 17 wa Jumuiya hiyo Jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli alisema hatua hiyo imetokana na mjadala na majadiliano ya kina kutoka kwa Wakuu wa Jumuiya hiyo. 
 Rais Magufuli alisema kwa mujibu wa mkataba huo, Umoja wa Ulaya ulitaka mkataba huo usainiwe mwaka huu, ambapo hata hivyo kwa kuzingatia maslahi na ustawi wa jumuiya hiyo, viongozi wa nchi wanachama wamehitaji muda zaidi wa kufanya maamuzi juu ya mkataba huo. 
 Dkt. Magufuli alisema kufuatia uamuzi huo, Viongozi hao wameitaka Sekretarieti ya Jumuiya hiyo kuandaa utaratibu wa kusimamia masuala ya mahusiano kuhusu mkataba huo kwa kufanya mawasiliano na Umoja wa Ulaya.
 “Tumewaomba wenzetu wa Umoja wa Ulaya wasiiadhibu nchi ya Kenya kwa kuwashinikiza kusaini mkataba wa EPA ifikapo oktoba mosi mwaka huu, ni vyema nchi zote wanachama tujiridhishe na vipengele vya mkataba huo kabla ya kuweka saini ya makubaliano” alisema Rais Magufuli. 
 Akitolea mfano baadhi ya sababu zinazoifanya nchi za Jumuiya hiyo kuhitaji muda zaidi wa majadiliano kuhusu mkataba huo ni pamoja na uhakika wa kulinda viwanda vya ndani vya nchi wanachama, njia bora za kulinda maslahi ya wakulima, namna bora ya makusanyo ya kodi za bidhaa kutoka nchi za Ulaya. 
 Kwa upande wake, Rais wa Uganda Yoweri Museveni alisema katika ulimwengu wa sasa suala la utengamano wa jumuiya unahitaji zaidi wingi wa watu na uwezo wa kujitosheleza kwa uzalishaji na masoko yatakayoyosaidia ukuaji wa uchumi kwa nchi wanachama. 
 “Mwaka 1960 idadi ya watu katika nchi za Afrika Mashariki ilikuwa na takribani watu Milioni 40 ukilinganisha na watu Milioni 165 waliopo sasa ambapo uwezo wa uzalishaji na masoko umeongezeka, hivyo hatuna budi kuwa na jumuiya yenye uwezo wa kuzalisha bidhaa kwa wingi na kutoa huduma” alisema Museveni. 
 Aidha Rais Museveni aliutaka Umoja wa Ulaya kukubaliana na uamuzi wa wakuu wa jumuiya hiyo kuwapa muda zaidi wa kufanya maamuzi kuhusu mkataba huo ambao umebeba maslahi mapana zaidi kwa wananchi wa jumuiya. 
 Naye Naibu Rais wa Kenya, William Ruto alisema maamuzi kuhusu mkataba huo yanalenga usawa na kuimarisha umoja baina ya nchi wanachama hivyo ili dhana hiyo iweze kwa wananchi ni wajibu wa Viongozi kuweka maslahi ya wananchi wao. 
 Katika mkutano huo, Wakuu wa Jumuiya hiyo walipokea ripoti mbalimbali ikiwemo ripoti ya mgogoro wa Burundi, ripoti ya mabaraza la mawaziri wa jumuiya hiyo kuhusu hali ya kisiasa inayoendelea nchini Sudan Kusini pamoja na uteuzi wa Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli na viongozi wenzie wakisimama wakati wimbo wa Jumuiya ukipigwa wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 17 wa Dharura wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki katika ukumbi wa mikutano wa Ikulu jijini Dar es salaam leo Septemba 8, 2016
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli akiongoza Mkutano wa 17 wa Dharura wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki katika ukumbi wa mikutano wa Ikulu jijini Dar es salaam leo Septemba 8, 2016
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli akihutubia Mkutano wa 17 wa Dharura wa Nchi za Jumuiya hiyo katika ukumbi wa mikutano wa Ikulu jijini Dar es salaam leo Septemba 8, 2016
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli akihutubia Mkutano wa 17 wa Dharura wa Nchi za Jumuiya hiyo katika ukumbi wa mikutano wa Ikulu jijini Dar es salaam leo Septemba 8, 2016
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Rais Dkt John Pombe Magufuli katika picha ya pamoja na viongozi wenzie baada ya Mkutano wa 17 wa Dharura wa Nchi za Jumuiya hiyo katika ukumbi wa mikutano wa Ikulu jijini Dar es salaam leo Septemba 8, 2016.

Kwa picha zaidi BOFYA HAPA

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...