Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amewataka wananchi wanaozunguka eneo la Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), kuwa watulivu katika kipindi hiki ambacho Serikali inatafuta ufumbuzi wa kudumu wa mgogoro kati yao na mwendeshaji wa uwanja huo kampuni ya KADCO.
Prof Mbarawa amesema ufumbuzi utakaopatikana utakuwa na manufaa kwa pande zote na kujali maslahi ya Taifa.
"Msiwe na wasiwasi Serikali yenu ni sikivu, tutayakagua maeneo yote na kuangalia maslahi ya pande zote na kutoa maamuzi yenye manufaa kwa wote", amesisitiza Prof. Mbarawa.
Mgogoro kati ya wananchi wanaozunguka uwanja wa ndege wa KIA na kampuni ya KADCO ambao umekuwako toka mwaka 1998 umesababisha misuguano na hisia kali kwa muda mrefu hali iliyosababisha Serikali kuamua kuupatia ufumbuzi wa kudumu.
Waziri Prof. Mbarawa ametuma timu ya wataalamu kupitia eneo lote la uwanja wa ndege huo lenye kilomita za mraba 110 katika siku mbili kuanzia sasa ili kuangalia wadau wote walioko ndani ya eneo hilo, athari zake kwa uwanja na wananchi kabla ya kutoa uamuzi wa mwisho.
Amezungumzia umuhimu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), kuilinda mipaka ya viwanja vyake na wananchi kujiepusha kuvamia maeneo ya viwanja ili kuepuka migogoro ya aina hiyo siku zijazo.
Katika hatua nyingine Prof. Mbarawa ameitaka KADCO kuongeza mapato katika uwanja wa ndege wa KIA ambao ni wa pili kwa ukubwa hapa nchini ili kuendana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kuongeza mapato katika sekta zote za kiuchumi.
Amesema nia ya Serikali ni kuboresha viwanja vyote vya ndege nchini ili kuimarisha huduma ya usafiri wa anga.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa KADCO Eng. Christopher Mukama amesema KADCO inajiendesha kwa faida na kuhakikisha inaendelea na uboreshaji wa huduma ili kuvutia ndege nyingi kutumia uwanja huo.
Waziri Prof. Mbarawa yuko mkoani Arusha kukagua ujenzi wa miundombinu unaoendelea mkoani humo.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, 
Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
 Muonekano wa jengo la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa pili kulia) mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), kuanza ziara ya siku mbili ya kukagua ujenzi wa miundombinu unaoendelea mkoani Arusha. Kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya KADCO Balozi Hassan Gumbo Kibelo.
 Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya KADCO Eng. Christopher Mukama akitoa taarifa ya utendaji wa kampuni hiyo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa tatu kushoto), mara baada ya kuwasili uwanjani hapo.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (katikati), akisisitiza jambo kwa uongozi wa Kampuni ya KADCO na watendaji wa Wilaya ya Hai. Kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya KADCO Balozi Hassan Gumbo Kibelo na kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Hai Bw. Gelasius Byakanwa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...