Mkuu wa Wilaya ya Arusha Mjini Mh. Gabriel Fabian Daqarro amelipongeza Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kwa kuendesha mafunzo maalum kwa waandishi wa Habari wa Mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara.

Mh. Gabriel Daqarro ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku moja ambayo yamefanyika Septemba 19 katika ukumbi wa Chuo cha Afya CEDHA mkoani Arusha.

“Ingawa mafunzo ni mafupi lakini napenda kulipongeza Shirika letu la Mafuta la Taifa kwa kuona umuhimu wa vyombo vya habari katika kupata uelewa mpana wa Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi ili waweze kuhabarisha na kuelimisha watanzania kwa ujumla ili watambue shughuli za shirika na faida zake haswa katika uchumi wa nchi”, alieleza Mkuu wa Wilaya.

Aidha Mh. Daqarro amewaomba Waandishi wa Habari kuwa wazelendo katika kuisaidia Serikali kutekeleza miradi mbalimbali yenye maslahi mapana katika maendeleo ya nchi yetu. ‘’Waandishi Wahabari mnapaswa kuisaidia Serikali katika utekelezaji wa miradi mbalimbali yenye tija kwa uchumi wa Taifa, mfano katika vita ya kiuchumi ya kugombania mradi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Uganda kati ya Tanzania na Kenya, wenzetu Kenya walijitahidi kuandika habari zenye kutoa wasifu wa nchi yao ili kuisaidia kupata mradi huo, hivi ndivyo mnavyopaswa kufanya kazi kiuzalendo.”

Aliongeza kuwa “leo hii mmeweza kuifahamu TPDC sasa mnapaswa kuwaeleza wananchi miradi inayofanywa na Shirirka hili na manufaa yake katika uchumi wa Taifa, mwende mkatafiti namna mradi wa bomba la mafuta utakavyonufaisha wananchi wanaoishi kando ya njia ya bomba hilo, vilevile namna bomba hilo litakavyosaidia kukuza uchumi wa nchi, hivi ndivyo tunavyoweza kujenga nchi yetu kupitia taaluma ya uandishi wa habari.”

Mkuu wa Wilaya alisisitiza kuwa ili tujenge Taifa imara ni vyema tuandike habari kwa weledi, uzalendo huku tukiondoa tofauti zetu za kiitikadi ziwe za kikabila, kisiasa au kidini kwa namna hii tutaweza kuandika habari zenye kujenga nchi yetu na si vinginevyo.

Hata hivyo Mwenyekiti wa Waandishi wa Habari Arusha ndugu ….pamoja na dhamira ya dhati ya Shirika katika utoaji wa elimu ya sekta ameliomba TPDC kutenga muda wa kutosha zaidi katika uelimishaji ili walengwa waweze kuelewa vyema sekta, ombi ambalo liliungwa mkono na Mkuu wa Wilaya.

Katika mafunzo hayo waandishi wa habari walipata fursa ya kujifunza kuhusu maendeleo ya Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi, Matumizi ya Gesi Asilia na Faida Zake, Mradi wa Bomba la Kusafirisha Mafuta Ghafi kutoka Uganda hadi Tanga na Usambazaji wa Gesi Asilia Majumbani, Viwandani na kwenye Vituo vya Kujaza Magari. 
Mkuu wa Wilaya ya Arusha Mjini Mh. Gabriel Fabian Daqarro akisisitiza umuhimu wa Waandishi wa Habari nchini katika kujenga uchumi wa nchi pale wanapotumia kalamu na taaluma yao kuelezea miradi inayotekelezwa na Serikali kwa maslahi ya taifa.
Mwanasheria wa TPDC ndg Goodluck Shirima akitoa mada ya Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi kutoka Uganda hadi Tanga kwa Waandishi wa Habari wa Mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro.
Waandishi wa Habari wa Mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara wakipata mafunzo ya masuala ya Mafuta na Gesi yaliyoandaliwa na TPDC.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...