Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameiagiza Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Nchi kuchunguza na kuwachukulia hatua kisheria na za kinidhamu viongozi na watumishi wa umma ambao wanakiuka taratibu za kazi kwa ajili ya maslahi yao binafsi.

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa kauli hiyo 8-Sep-2016 mjini Mtwara wakati anafungua jengo la sekretarieti ya maadili ya viongozi wa umma Kanda ya Kusini ambalo ujenzi wake umegharimu takribani shilingi bilioni MBILI.

Makamu wa Rais amesema iwapo kama hatua hizo zitachukuliwa haraka zitakomesha na kupunguza kasi ya mmomonyoko wa maadili kwa viongozi na watumishi wa umma hali ambayo itaongeza uwajibikaji katika utendaji wa kazi miongoni watendaji hao.

Amesisitiza kuwa serikali itaendelea kuiimarisha sekretarieti ya maadili ya viongozi wa umma nchini kwa kuijengea uwezo wa rasilimali watu na fedha kwa kadri hali ya uchumi itakavyo ruhusu ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Makamu wa Rais amewahimiza viongozi na watumishi wa umma kuthamini na wahakikishe walinda maslahi ya umma wakati wote wa utendaji wao wa kazi ili kuondoa malalamiko kwa wananchi.

Makamu wa Rais amesema ni jambo la muhimu kwa sekretarieti hiyo kufutilia mienendo ya viongozi wa umma na kuwabaini wale wanaokwenda kinyume na misingi ya uadilifu na wachukuliwe hatua ipasavyo kabla hawaleta madhara kwa serikali na jamii kwa ujumla.

Makamu wa Rais pia ametoa rai maalum kwa wananchi wa mkoa wa Mtwara kuitumia ofisi hiyo mpya ya sekretarieti ya maadili ya viongozi wa umma Kanda ya Kusini kwa kutoa taarifa kuhusu mienendo ya viongozi wanaokiuka maadili ya umma katika utendaji wao wa kazi ili waweze kuchukuliwa hatua.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala bora Angela Kairuki amesisitiza kuwa kazi ya kuhakiki mali na madeni ya viongozi wa umma itaendelea kwa kasi nchini na mwaka huu sekretarieti hiyo itahakiki mali za viongozi wapatao 500 kote nchini.

Naye Jaji Mstaafu na Kamishna wa Maadili Nchini Salome Kaganda akitoa taarifa kuhusu ujenzi wa jengo hilo ameiomba serikali itenge fedha za kutosha kwa ajili ya kufanikisha zoezi la uhakiki wa mali na madeni ya viongozi kwa nchi nzima.

Imetolewa na 
Ofisi ya Makamu wa Rais 
Mtwara.
8-Sep-2016.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...