Mkuu wa Chuo cha Takwimu Mashariki mwa Afrika (EASTC) Prof. Innocent
Ngalinda amezindua mafunzo maalumu ya Ukusanyaji Takwimu Rasmi ambayo
yalianza tarehe 17 Oktoba mwaka huu chuoni Changanyikeni jijini Dar es Salaam.
Akizungumza leo wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo, Prof. Ngalinda amesema
mafunzo hayo yameandaliwa kwa nia ya kumpatia mshiriki ujuzi katika ukusanyaji
takwimu kwa ajili ya kuzichakata na kuwa takwimu rasmi.
“Washiriki hawa watafundishwa mbinu shirikishi, utatuzi wa matatizo mbalimbali
wakati wa ukusanyaji takwimu, sensa na viwango vya tafiti mbalimbali, utunzaji
wa Vifaa vya ukusanyaji takwimu kama vile simu za mkononi na kumpyuta
mpakato pamoja na kubadilisha madodoso ya kawaida na kuwa ya kisasa”,
amesema Prof. Ngalinda.
Akizungumzia malengo ya mafunzo hayo Naibu Mkuu wa Chuo, Taaluma, Utafiti
na Ushauri wa Kitaalamu wa chuoni hapo Dkt. Frank Mkumbo amesema lengo ni
kuwawezesha wakusanyaji takwimu kukusanya takwimu halisi na zenye ubora
kwa ajili ya kupanga mipango mbalimbali ya Maendeleo.
“Lengo kuu la mafunzo haya ni kuhakikisha kuwa wakusanyaji takwimu rasmi
wanakuwa na weledi wa kutosha katika kukusanya takwimu bora na zenye tija kwa
taifa” amefafanua Dkt. Mkumbo.
Jumla ya washiriki 110 wamejiunga na mafunzo hayo maalumu ya muda wa miezi
miwili kwa awamu ya kwanza ambayo yatamalizika mwezi Disemba, 2016 na
watakaomaliza na kufaulu watapatiwa cheti cha Ukusanyaji Takwimu. Awamu ya
pili ya mafunzo hayo yanatarajiwa kuanza Novemba mwaka huu na kumalizika
Januari, 2017.
Mkuu wa Chuo cha Takwimu Mashariki mwa Afrika
(EASTC) Prof. Innocent Ngalinda akizungumza na washiriki wa mafunzo na
waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa mafunzo maalumu
ya Ukusanyaji Takwimu Rasmi uliofanyika leo katika chuo hicho kilichopo
Changanyikeni jijini Dar es salaam.
Naibu Mkuu wa Chuo, Taaluma, Utafiti na Ushauri wa
Kitaalamu wa Chuo cha Takwimu Mashariki mwa Afrika (EASTC) Dkt. Frank
Mkumbo akizungumza na washiriki wa mafunzo na waandishi wa habari wakati
wa uzinduzi wa mafunzo maalumu ya Ukusanyaji Takwimu Rasmi uliofanyika leo
katika chuo hicho kilichopo Changanyikeni jijini Dar es salaam.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo maalumu ya Ukusanyaji
Takwimu Rasmi wakimsikiliza kwa makini Mkuu wa Chuo cha Takwimu
Mashariki mwa Afrika (EASTC) Prof. Innocent Ngalinda wakati wa uzinduzi wa
mafunzo hayo uliofanyika leo katika chuo hicho kilichopo Changanyikeni jijini
Dar es salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...