Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango

Benny Mwaipaja, MoFP, Washington DC, Marekani
SERIKALI ya Japan, kupitia Shirika lake la Maendeleo-JICA, imeahidi kuongeza kiwango cha ruzuku kwa serikali ya Tanzania ili kufadhili miradi mbalimbali ikiwemo kilimo, Maji, miundombinu ya barabara na huduma nyingine za jamii ili kuisaidia kufikia maendeleo yaliyokusudiwa kwa wananchi wake.

Ahadi hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Japan-JICA, Hiroshi (Hiro) Kato, alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, Jijini Washington DC, nchini Marekani.

“Kabla ya mwaka 2013 tulikuwa tunatoa ruzuku ya dola milioni 1 kwa Tanzania kila mwaka, lakini kuanzia mwaka 2013 tumeongeza kiwango hadi kufikia dola milioni mia 3 kila mwaka na tunatarajia kuongeza kiwango hicho siku za hivi karibuni” aliongeza Makamu huyo wa Rais wa JICA
Kato amesema kuwa Tanzania na Japan ni marafiki wa muda mrefu na kwamba nchi hiyo itaendelea kuisaidia kwa kutekeleza miradi mbalimbali yenye kuleta tija kwa uchumi wa nchi na maisha ya watanzania kwa ujumla.

“Hivi sasa tunataka kuanza kutekeleza awamu nyingine ya mradi wa kilimo cha umwagiliaji cha zao la mpunga ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo ambalo ni muhimu sana” Aliongeza Kato.

Amesema kuwa Japan pia imeamua kuongeza kiwango cha ufadhili kwa Bara la Afrila kutoka Dola Milioni 13 ambazo nchi hiyo ilikuwa ikitoa kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2013 hadi kufikia dola elfu 30 kwa mwaka kuanzia mwezi Agosti, 2016 kwa kipindi cha miaka 3 ijayo.

Amesema pia kuwa ili kuwajengea uwezo na ujuzi vijana wa kiafrika, Japan imeanzisha program ya kutoa elimu ambapo hivi sasa vijana 60 kutoka nchi mbalimbali za kiafrika wamepelekwa nchini humo kujifunza kwenye vyuo vilivyoko huko na watapelekwa kwenye kampuni na mashamba makubwa yanayojihusisha na kilimo ili waweze kupata uzoefu na kuwa chachu ya mabadiliko watakaporejea katika nchi zao.

Akiongea na Makamu huyo wa Rais wa Shirila la Maendleo la Japan-JICA, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, ameishukuru Japan kwa kuisaidia Tanzania katika Nyanja mbalimbalimbali za kiuchumi na kijamii.

Ametaja baadhi ya miradi ambayo nchi hiyo inafadhili nchini Tanzania kuwa ni ujenzi wa barabara ya Arusha hadi Holili hadi Taveta nchini Kenya, Ujenzi wa barabara ya Juu (Flyover) ulioanza eneo la Tazara ili kupunguza msongamano Jijini Dar es salaam, miradi ya maji na kilimo cha umwagiliaji.

“Asilimia 75 ya wananchi wetu wanategemea kilimo kwahiyo uamuzi wa Japan wa kuwekeza fedha nyingi kwenye miradi ya kilimo cha umwagiliaji ni jambo tunalolipongeza kwasababu kilimo kitakuwa na tija na kitaendeshwa kibiashara” Alisema Dkt. Mpango.

Ameishukuru pia serikali ya Japan kwa kufanya utafiti na upembuzi yakinifu wa mradi wa kudhibiti mafuriko ya mto Kondoa, eneo la mkoa wa Morogoro ili kudhibiti mto huo usiharibu miundombinu ya reli ya kati.

“Mradi huu ni muhimu sana kwasababu serikali imekuwa ikiingia hasara karibu kila mwaka kukarabati njia hiyo ya reli baada ya kusombwa na maji, hivyo tunaishukuru Japan kwa kutusaidia kufanya utafiti huo ambao utasaidia kukabiliana na hali hiyo” aliongeza Dkt. Mpango
Ameahidi kuwa serikali ya awamu ya tano imejipanga kukusanya kodi na kuziba mianya ya upotevu wa fedha za serikali ikiwemo kuanzisha mahakama maalumu ya kushughulika na mafisadi ili kuleta nidhamu katika utumishi wa umma.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...