Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 03 Oktoba, 2016 amekutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais wa Cuba Mhe. Salvador Antonio Valdes Mesa ambapo viongozi hao wamekubaliana kuimarisha na kuongeza uhusiano na ushirikiano kati ya nchi hizi mbili kwa manufaa ya wananchi wake.

Katika Mazungumzo hayo Rais Magufuli amesema anatambua uhusiano na ushirikiano mzuri na wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Cuba na kwamba Serikali yake imejipanga kuhakikisha uhusiano huu unaelekezwa katika maeneo yenye manufaa ya kiuchumi na ustawi wa jamii.

Rais Magufuli amemuomba Makamu huyo wa Rais wa Cuba kuwashawishi wawekezaji wa kutoka nchini mwake kuja hapa nchini kujenga viwanda vya kutengeneza dawa za binadamu ili kurahisisha upatikanaji wa dawa na kupunguza gharama.

Pia, Rais Magufuli amemuomba Makamu wa Rais wa Cuba Mhe. Salvador Antonio Valdes Mesa kuwashawishi wafanyabiashara wa Cuba kuja kuwekeza katika uzalishaji wa sukari na amewahakikishia kuwa wakiwa tayari Serikali ya Tanzania ipo tayari kuwapa ardhi kwa ajili ya kuendesha uzalishaji huo.

"Mhe. Salvador Antonio Valdes Mesa najua kuwa nchi yenu ina utaalamu wa kutosha katika uzalishaji wa sukari, uzalishaji wa dawa za binadamu na masuala mengine mengi yanayohusu matumizi ya teknolojia katika shughuli mbalimbali za uzalishaji, nakuomba uwaambie wafanyabiashara wa Cuba kuwa tunawakaribisha waje Tanzania kuwekeza na Serikali itawapa ushirikiano wa kutosha" amesema Rais Magufuli.

Kwa upande wake Makamu wa Rais wa Cuba Mhe. Salvador Antonio Valdes Mesa amempongeza Rais Magufuli kwa juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali yake katika kuinua uchumi wa Tanzania na amemhakikishia kuwa Cuba ipo tayari kushirikiana na Tanzania kwa kutumia utaalamu na uzoefu wake.

Amesema kwa kuanzia Cuba italeta wataalamu kwa ajili ya kuangalia namna itakavyotekeleza ombi la kujenga viwanda vya kutengeneza dawa za binadamu na pia atazungumza na Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Cuba na kuwashawishi kuja hapa nchini kuwekeza katika uzalishaji wa sukari.

"Mhe. Rais Magufuli natambua kuwa uhusiano wetu na Tanzania na Afrika ni wa kihistoria, sisi Cuba tumepiga hatua kubwa katika maendeleo ya uchumi na teknolojia, nimekuja kukuhakikishia kuwa tutauendeleza uhusiano huu ili ulete manufaa kwenu na kwa wananchi wa Cuba" amesema Mhe. Mesa.


Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
03 Oktoba, 2016
Rais Dkt. John Pombe Magufuli akiwa katika mazungumzo na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Cuba, Salvador Antonio Valdes Mesa (kulia kwake) na ujumbe wake alipokutana nae Ikulu jijini Dar es salaam leo Oktoba 3, 2016. Makamu wa Rais wa Cuba, yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu yenye lengo la kuendeleza na kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Cuba katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, utamaduni, michezo, kilimo, nishati, teknolojia na kuangalia maeneo mapya ya uwekezaji.
Makamu wa Rais, Mh. Samia Suluhu Hassan (wa tatu kulia walioketi) akiwa na mgeni wake Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Cuba, Salvador Antonio Valdes Mesa (wa tatu kushoto walioketi) wakiwa katika picha ya pamoja na ujumbe wao, mara baada ya mazungumzo, Ikulu jijini Dar es salaam leo Oktoba 3, 2016.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimkabidhi zawadi ya picha ya kuchora Makamu wa Rais wa Cuba Salvador Valdes Mesa kabla ya kumkabidhi kama zawadi Ikulu.

Makamu wa Rais wa Cuba Salvador Valdes Mesa akimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli mara baada ya kumaliza mazungumzo yao Ikulu jijini Dar es Salaam.

PICHA ZAIDI BOFYA HAPA 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...