Dkt Masaburi enzi za uhai wake
Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameitumia salamu za rambirambi
familia ya Meya Mstaafu wa Jiji la Dar es Salaam Dkt. Didas Masaburi
aliyefariki dunia jana tarehe 12 Oktoba, 2016 katika Hospitali ya Taifa
Muhimbili Jijini Dar es Salaam.
Katika salamu hizo
Rais Magufuli amesema amepokea taarifa ya kifo cha Dkt. Didas Masaburi kwa
mshituko na masikitiko makubwa na kwamba anaungana na familia ya marehemu,
ndugu, jamaa na marafiki katika kipindi hiki kigumu cha huzuni ya kuondokewa na
mpendwa wao.
"Poleni sana
familia ya Dkt. Didas Masaburi, najua huu ni wakati mgumu sana kwenu, lakini
niwahakikishie kuwa sote tumeguswa sana na msiba huu kwa kuwa tumempoteza mtu
muhimu, msomi mzuri, kiongozi aliyelitumikia Taifa kwa moyo wake wote na
aliyesimamia kile alichokiamini" amesema
Rais Magufuli katika salamu hizo.
Aidha, Dkt.
Magufuli amewapa pole wanachama na wapenzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao
wamempoteza Mwana-CCM mwenzao pamoja na Viongozi na watumishi wa Jiji la Dar es
Salaam ambao walifanya nae kazi alipokuwa Meya wa Jiji.
Amemuombea kwa
Mwenyezi Mungu ampumzishe mahali pema peponi.
"Bwana alitoa
na Bwana ametwaa, jina lake lihimidiwe. Amina"
amemalizia Rais Magufuli.
Gerson
Msigwa
Mkurugenzi
wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es
Salaam
13 Oktoba,
2016
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...